Joy FM

WCF yatoa viti mwendo kusaidia wenye mahitaji maalum Kasulu

22 October 2025, 09:51

Muonekano wa viti mwendo vilivyokaliwa na watu wenye mahitaji maalum ambavyo vimetolewa na WCF, Picha Hagai Ruyagila

Watu wenye mahitaji maalum hawana budi kushirikishwa kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi ikiwa ni sehemu ya kujenga jamii jumuishi

Na Hagai Ruyagila

Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umetoa msaada wa viti mwendo 11 vyenye thamani ya shilingi milioni 4.5 kwa Shirika la Sauti Yetu Foundation kwa ajili ya kuwagawia watu wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma.

Hafla ya ugawaji wa viti mwendo imefanyika katika ukumbi wa mikutano wa shule ya sekondari Bongwe iliyopo Mjini Kasulu na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wawakilishi wa taasisi pamoja na wanufaika wa msaada huo.

Akizungumza katika hafla hiyo Kaimu Mkurugenzi wa Sauti Yetu Foundation kutoka jijini Dodoma BW. Raphael Mabula amesema msaada huo unalenga kuwawezesha watu wenye mahitaji maalum kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi ikiwa ni sehemu ya juhudi za kujenga jamii jumuishi isiyomwacha mtu nyuma.

Kaimu Mkurugenzi wa Sauti Yetu Foundation kutoka jijini Dodoma BW. Raphael Mabula, Picha na Hagai Ruyagila

Kwa upande wake, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mji Kasulu Mwl, Vumilia Simbeye ambaye alikuwa Mgeni rasmi katika tukio hilo amelipongeza shirika hilo kwa moyo wao wa huruma na upendo kwa jamii hususan kwa watu wenye mahitaji maalum.

Amewasihi pia wazazi na walezi kutowaficha watoto wao wenye ulemavu majumbani, bali wawape fursa ya kushiriki katika shughuli za kijamii na kupata haki sawa na watoto wengine.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mji Kasulu Mwl, Vumilia Simbeye, Picha na Hagai Ruyagila

Baadhi ya wazazi na walezi wa watoto waliopokea msaada huo akiwemo Amina Bakari wametoa shukrani zao za dhati kwa shirika hilo kuwa msaada huo umewapa matumaini mapya na kuongeza uwezo wa watoto wao kushiriki katika maisha ya kila siku.

Baadhi ya wazazi na walezi wa watoto wenye mahitaji maalum waliopewa viti mwendo wakiwa katika picha na Hagai Ruyagila

Shirika la Sauti Yetu Foundation linaendelea na juhudi zake za kuwasaidia watu wenye uhitaji katika maeneo mbalimbali nchini likilenga kuboresha maisha na kutoa fursa sawa kwa makundi yote ya jamii.