Joy FM

Wanafunzi wenye ulemavu wapewa bima za afya Kasulu

6 August 2025, 12:33

Mkuu wa Wilaya Kasulu akiwa ameshika kadi za bima ya afya na kuzikabidhi kwa walimu zilizotolewa na taasisi ya Usilie Tena, Picha na Hagai Ruyagila

Wito umetolewa kwa wadau mbaimbali na mashirika kuendelea kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalumu ili waweze kufikia ndoto zao.

Na Hagai Ruyagila

Katika kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita katika kuboresha sekta ya afya nchini, Taasisi ya Usilie Tena yenye makao yake makuu jijini Dar es Salaam, imetoa msaada wa kadi za bima ya afya kwa baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Rungwe Mpya na Kalema, zilizopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Bi. Egra Kamugisha, amesema hatua hiyo inalenga kusaidia wanafunzi wenye mahitaji maalumu ambao wanakumbwa na changamoto ya kukosa huduma bora za afya kutokana na hali ngumu ya maisha.

Sauti ya Mkurugenzi wa Taasisi ya Usilie Tena Bi. Egra Kamugisha
Mkurugenzi wa taasisi ya Usilie Tena Bi. Agra Kamugisha, Picha na Hagai Ruyagila

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isaac Mwakisu ameishukuru Taasisi hiyo kwa moyo wa huruma waliouonesha kwa watoto hao, na kumuombea heri mkurugenzi wa taasisi hiyo kwa kazi njema anayofanya kwa jamii.

Sauti ya Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isaac Mwakisu

Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Kalema, Mwalimu Hellena Kabonye, pamoja na Mwalimu wa Kitengo cha Elimu Maalum kutoka Shule ya msingi Rungwe Mpya, Mwalimu Agatha Chendro, wamesema msaada huo wa bima ya afya utasaidia kwa kiasi kikubwa kuinua kiwango cha ufaulu wa wanafunzi hao kwa kuwa hawatalazimika kukosa masomo kutokana na maradhi.

Sauti za Walimu wa wanafunzi waliopewa bima za afya

Baadhi ya wazazi na watoto waliopokea bima hizo wameonesha furaha na kutoa shukrani kwa mdau huyo wa elimu, huku wakihimiza malezi bora na kuhakikisha watoto wote wanapata elimu bila vikwazo.

Sauti ya baadhi ya wazazi na watoto waliopokea bima za afya
Mkuu wa Wilaya Kasulu akiwa ameshika kadi za bima ya afya na kuzikabidhi kwa walimu zilizotolewa na taasisi ya Usilie Tena, Picha na Hagai Ruyagila

Hatua hii ya Taasisi ya Usilie Tena ni mfano hai wa ushirikiano kati ya serikali na wadau binafsi katika kuhakikisha kila mtoto anapata haki ya msingi ya afya na elimu, hasa wale wenye uhitaji maalum.