Joy FM
Joy FM
7 November 2025, 08:51

Baadhi ya vijiji yatakapojengwa masoko hayo ni Simbo wilayani Kigoma, Kazuramimba na Nguruka wilayani Uvinza na Rusesa, Kasangezi na Bugaga wilayani Kasulu.
Na Emmanuel Matinde
Serikali Mkoani Kigoma imeanza mpango wa ujenzi wa masoko madogo ya wachuuzi kwenye vituo vidogo vya mabasi vilivyoko kando ya barabara katika baadhi ya vijiji mkoani humo ili kuwaondolea adha ya mvua na jua wananchi wanaofanya biashara ndogo ndogo za mazao ya kilimo kwa abiria wa mabasi katika maeneo hayo.
Ujenzi wa masoko hayo utakaogharimu takribani Shilingi Milioni 500 ambazo ni ufadhili kutoka Shirika la Maendeleo la Watu wa Ubelgiji (ENABEL), unatarajiwa kukamilika katika kipindi cha mwezi mmoja kutoka sasa.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa, amesema hatua hiyo inalenga kuwawekea mazingira rafiki wajasiriamali hao wadogo ya kujikwamua kiuchumi, ambao wengi wao ni vijana, wanawake na watu wenye ulemavu ikiwa ni sehemu ya kutumia kwa ufanisi hifadhi ya barabara.
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro, ametembelea na kukagua hatua za ujenzi wa masoko hayo, kisha kuzungumza na wananchi.

Katibu Tawala Msaidizi Miundombinu Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhandisi Fransisco Magoti, amesema masoko hayo yatajengwa katika maeneo tofauti 14, huku baadhi ya walengwa wakifurahia hatua hiyo.