Zenj FM
Zenj FM
4 April 2025, 4:35 pm

Na Mary Julius.
Waziri wa Nchi Afisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Sharif Ali Sharif, amesema kuanza kutumika kwa mfumo wa kidijitali wa utoaji wa mikopo kwa makundi maalum 4.4.2 kutarahisisha upatikanaji wa mikopo, haraka na usalama.
Ameyasema hayo wakati akizindua mfumo wa kidijitali wa utoaji wa mikopo kwa makundi maalum 4.4.2. hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Dk.Shein ZURA Maisara.
Waziri Sharif amesema changamoto kubwa katika utoaji wa mikopo hiyo ilikuwa ni utaratibu mrefu wa kupata mikopo, ambapo ucheleweshaji na urasimu vilikuwa vikichelewesha upatikanaji wake kwa wajasiriamali mfumo hivyo kuzinduliwa kwa mfumo huo wa kidijitali kutasaidia kurahisisha upatikanaji wa mikopo kwa njia ya uwazi, urahisi, na usalama zaidi na kuondoa changamoto zote za awali.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (ZEEA), Juma Burhan Mohammed amesema kuwepo kwa mfumo huu kutakuwa mwarubaini wa kutatua changamoto ya ucheleweshaji wa mikopo na ulejeshwaji wa mikopo hiyo.
Nae Mtendaji Mkuu wa Tanzania Commercial Bank, Jema Msuya, amesema TCB wanajivunia kuwa sehemu ya ufanikishaji wa mfumo wa kidijitali wa utoaji wa mikopo kwa makundi maalum 4.4.2.na anatarajia mfumo huo utaongeza ufanisi, uwazi, na urahisi katika utoaji wa mikopo.
Mkurugenzi Mkakati Kampuni ya AirPay,Mihayo Wilmore, Ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuwaamini na kuwapa kazi ya kutengeneza uchumi jumuishi wa kidijitali.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu,Ussi Khamis Debe amesema kuwepo kwa mfumo huo utasaidia kundi la watu wenye ulemavu kupata mikopo kwa urahisi zaidi.
Mfumo wa kidijitali wa utoaji wa mikopo kwa makundi maalum 4.4.2 unatarajiwa kuanza kufanya kazi rasmi April 15 mwaka huu.