Zenj FM

Mahakama maalum Zanzibar mwarobaini vitendo vya udhalilishaji

27 November 2023, 7:31 pm

Raisi wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi akifungua mahakama ya udhalilishaji Zanzibar.

Kwa miaka mingi Zanzibar, vitendo vya ukatili wa kingono na ukatili wa kijinsia (SGBV) vimekuwa vikifanywa bila ya kuadhibiwa.

Na Ivan Mapunda.

Mwaka 2002 kwa mfano, TAMWA ilipokea ripoti kutoka Mahakama Kuu ikionesha 0% ya hatia dhidi ya kesi 200 zilizofunguliwa yaani kati ya kesi 200 zilizofikishwa mahakamani hakuna tuhuma iliyotiwa hatiani.

Aidha katika ngazi ya jamii, kulikuwa na kiwango cha juu cha unyanyapaa unaohusishwa na SGBV, kadhalika wanajamii walijawa na hofu na kuogopa athari au adhabu watakazozipata kutoka kwa wanajamii wenzao pindipo wanapoziripoti kesi hizo.

 Wakati huo huo, kulikuwa na kesi nyingi ambazo zilitatuliwa katika ngazi ya familia.

Januari 2021 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Dk Hussein Ali Mwinyi alitangaza kwa umma umuhimu wa kuanzishwa kwa mahakama maalum kama hatua ya kukabiliana na vitendo vya udhalilishaji Zanzibar na akasema kuwa;

Sauti ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Dk Hussein Ali Mwinyi

Kwa kuzingatia hilo, ilipofika june, 2021, mahakama maalum ilianzishwa rasmi.

Mahkama ambayo inashughulikia kesi za uidhalilishaji.

Ili kujua mengi kuhusiana na mafanikio na changamoto tangu kuanzishwa rasmI kwa Mahakama Maalum june  2021  ungana nami Ivan Mapunda kusoma makala hii inayoangalia utendaji kazi wa mahakama maalum hapa zanzibar.

Tangu kuanzishwa rasmi kwa Mahakama Maalum june 2021 Zenj fm imezungumza na baadhi ya wanachi  ambao wamesema mahakama imekua ikifanya kazi nzuri japo kuwa kuna changamoto ya wananchi walio wengi kutokuridhishwa na huduma inayotolewa na mahkama maalum kuhusu hukumu zinazotolewa kutokuwatia watuhumiwa hatiani kutokana na sababu mbalimbali.

kwa upande wake Moja ya mwananchi  ameiambia zenj fm kuwa moja ya sababu kubwa  ambayo inakwamisha kesi nyingi  ni ushahidi kwamba shahidi aliyeona tukio haruhusiwi kutoa ushahidi pamoja na  (mshtakiwa) hakuitwa mahakamani hadi kesi ilipotupiliwa mbali  jambo ambalo linavunja moyo na jamii kukosa imani na mahakama maalum.

Mfano wa kutoridhika kwa mwenendo wa kesi

Mama Maryam Khamis Mkaazi wa Mpapa Kaskazini Unguja alieleza kuwa mjukuu wake (7) anayeishi naye alibakwa na mtoto wa jirani yake julai 2020 na kufikisha suala hilo kituo cha polisi Dunga.

Faili la kesi ya mjukuu wake lilitumwa kwa ofisi ya mwendesha mashtaka wa umma na kisha kupelekwa mahakamani, lakini cha kushangaza hawajawahi kuitwa kutoa ushahidi kuhusu suala hilo.

Alisema kuwa alikwenda kuuliza kuhusu kesi ya mjukuu wake katika kituo cha polisi na aliambiwa kuwa faili tayari limepelekwa kwa dpp. Alipoenda kwa dpp, aliambiwa asubiri ikiwa tayari watampigia simu.

Hivyo alisema alikuwa akirushwa kati ya polisi na DPP bila kupata msaada wowote na julai 2021 alipokwenda kwaDPP kuuliza kuhusu kesi hiyo, aliambiwa kuwa kesi ya mjukuu wake ilifutwa, alipouliza kwa nini hajapelekwa. Alipopigiwa simu kutoa ushahidi, aliambiwa kuwa simu yake haipatikani.

Lakini pia wananchi hao walizungumzia swala la ushirikiano kati ya wahasiriwa na wasimamizi wa sheria  ambapo wahojiwa wengi walisema kuwa walipata ushirikiano mzuri kutoka kwa wasimamizi wa sheria, polisi, DPP na mahkama.

Asilimia 65 ya wahojiwa walisema kuna ushirikiano mzuri.  Asilimia 35 walisema hakuna ushirikiano.

Aidha jamii  imetakiwa kutomaliza kesi za udhalilishaji katika ngazi ya familia kwani Kufanya hivyo ni kumnyima haki yake ya msingi muathirika na kuendelea kumdhalilisha na hatimaye kumpa ugonjwa wa milele wa kiakili na kimwili.

Sambamba na  hilo jamii inapaswa kuwa karibu na watoto chini ya umri wa miaka 18 hivyo kuelewa mapema iwapo kuna jambo lolote baya litawatokea, kwa sababu wahusika wengi wa matukio hayo ni wanafamilia wa karibu, hivyo kitendo cha kuchelewa kumgundua mtoto aliyefanyiwa ukatili huo. Husababisha ugumu wa kupata ushahidi.

Zenj fm iligonga hodi katika ofisi za  mahakma ya mkoa na kuzungumza na Hakimu wa Mahakama ya Mkoa Sara Omar Hafidh  na kutaka kujua mchango wao mkubwa katika kuhakikisha mahakama  hiyo inatoa haki  alisema katika kuchangia ufanisi wa mahkama hiyo maalum wanahakikisha wanatekeleza vyema wajibu wao wa kikatiba na kisheria wa kuendesha kesi kwa ufanisi na kwa mujibu wa sheria; kuita mashahidi haraka na kuhakikisha kuwa kesi hazicheleweshwi.

Lakini pia zenj fm hakuishia hapo tu ilitaka kujua kuna changamoto gani ambayo inapelekea kesi nyingi zinazopelekwa mahakamani hapo kufutwa  na kumalizika mapema akajibu kuwa kesi nyingi zinazomalizika mapema watuhumiwa wanaachiwa huru kwa ukosefu wa ushahidi, hivyo ndiyo kusema kuwa kuna changamoto katika eneo la upelelezi.

Sauti ya Hakimu wa Mahakama ya Mkoa Sara Omar Hafidh

Pia mahakama  zilisema siku hizi kesi hazichukui muda mrefu, kwa sababu faili hupelekwa mahakamani ndani ya wiki mbili na taratibu za mahakama huanza na kwa kawaida ndani ya miezi miwili kesi hupata hukumu. Zimesema mara nyingi ucheleweshaji wa kesi hutokea hasa kipindi ambacho  Shahidi daktari au mpelelezi kama amekwenda likizo au kozi ya mafunzo Pamoja na mashahidi/wahasiriwa kutofika mahakamani.

Sauti ya Hakimu wa Mahakama ya Mkoa Sara Omar Hafidh

Mfano wa kesi kucheleweshwa.

Mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 11 anayeishi mwanyanya mjini magharibi alitekwa nyara na kijana wa miaka 25. Tukio lilitokea mwaka 2019, na kesi hiyo kufunguliwa mahakamani tarehe 31/06/2021, kesi na. 140/2021 na hukumu ilitolewa tarehe 01/08/2023, ambapo mshitakiwa ameachiwa huru.

Mama wa mtoto huyo alisema kuwa kesi hiyo iliahirishwa zaidi ya mara 4. Hukumu ilipotoka, mtuhumiwa aliachiwa huru. Mama huyo amepoteza imani na mahakama na hali hiyo imemuathiri kisaikolojia.

Baya lazima lisemwe na zuri lazima lisifiwe ndipo na sisi zenj fm tukatoa maua yetu kwa mahakama maalum kuangalia mfanikio mbali na changamoto hizo ila yapo mafanikio ya uwepo wa mahakama maalum ya udhalilishaji ni pamoja na kuongeza kasi ya usikilizwaji wa kesi za udhalilishaji katika mahakama hizo na angalau hukumu zinazotolewa ni za kuridhisha ikilinganishwa na kabla ya kuanzishwa kwa mahakama hiyo maalum.

Pamoja na kwamba utamaduni wa usiri bado upo katika jamii lakini umepungua kidogo kutokana na mwamko unaotolewa na asasi za kiraia pamoja na serikali.

Kwa upande mwingine, ukosefu wa vifaa katika mahakama na miundombinu duni bado ni changamoto, mfano majengo ya mahakama ya Vuga, Mahonda, Mkoani na Wete Pemba ni ya zamani.

Aidha, tatizo la mashahidi kutofika mahakamani kutoa ushahidi linatakiwa kuangaliwa kwa jicho la tatu kwa sababu uchunguzi umeweza kubaini kuwa kesi nyingi zimefutwa kwa kukosa ushahidi jambo ambalo linarudisha nyuma juhudi za kupambana na sgbv.

Ndugu zangu wananchi,wazazi walezi tuchukue hatua ya kuwalinda watoto wetu wakiume na wakike na kufutilia nyendo zao tuache tabia  ya huchukulia matukio ya unyanyasaji wa kingono kama chanzo cha mapato. Wengine hutoa mashtaka ya uwongo kwa baadhi ya watu ili kulipiza kisasi, zanzibar bila ukatili wawatoto na wanawake inawezekana tupaze sauti zetu usichukulie poa.