Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
31 July 2026, 15:17

Polisi wa Usalama Barabarani wamewapa elimu wamiliki na madereva wa matrekta na power tiller katika Kata ya Chita, huku wakisisitiza marekebisho ya vyombo hivyo na ufuataji wa taratibu za usajili na leseni ili kupunguza ajali.
Na: Isidory Mtunda
Wamiliki na madereva wa matrekta na power tiller katika Kata ya Chita, Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba mkoani Morogoro, wameiomba Timu ya Usalama Barabarani kuwapa muda wa kurekebisha dosari zilizopo kwenye vyombo vyao ili kupunguza ajali zinazochangiwa na matumizi ya vyombo hivyo.

Maombi hayo yametolewa wakati wa mafunzo ya usalama barabarani yaliyotolewa na Timu ya Usalama Barabarani iliyoongozwa na ASP Blandina Kasongwa, yenye lengo la kuwajengea uelewa wamiliki na madereva kuhusu matumizi salama ya matrekta na power tiller.

Kwa upande wake, Mkaguzi wa Magari wa Wilaya ya Kilombero, Sajenti Rajabu Kadikarange, amefafanua kuhusu utaratibu wa upatikanaji wa leseni za udereva. Amesema madaraja ya leseni kama E na C yanapatikana baada ya dereva kuwa na uzoefu wa angalau miaka mitatu, hivyo haiwezekani kuruka kutoka daraja la awali na kwenda moja kwa moja kusomea madaraja hayo.

Akihitimisha mafunzo hayo, ASP Blandina Kasongwa amewaagiza wamiliki na madereva wote kujiorodhesha ili idadi yao itambuliwe kwa urahisi. Aidha, amesisitiza kuwa Jeshi la Polisi halipokei fedha za mafunzo wala ada za leseni, na kwamba malipo yote yanapaswa kufanyika kupitia Control Number zilizotolewa na mamlaka husika.