Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
24 June 2026, 19:56

Viongozi na watendaji wa ushirika watakiwa kuchukua hatua madhubuti za kuzuia vitendo vya rushwa ili kuongeza ufanisi katika utendaji na kuimarisha imani ya wanachama
Na Katalina Liombechi
Uwepo wa baadhi ya watendaji na wajumbe wa bodi wasio waaminifu pamoja na ubovu wa miundombinu ya barabara imetajwa kuwa ni miongoni mwa changamoto zinazoikabili sekta ya ushirika katika Mkoa wa Morogoro.
Hayo ni kwa mujibu wa mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Bertha Mwanzalima, amewasilisha taarifa kuhusu hali ya ushirika katika Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Morogoro 2026 ambalo linafanyika Ifakara kwa siku mbili kuanzia leo June 24,2026 katika ukumbi wa Vunjabei likiwa na lengo la kujadili fursa,mafanikio,changamoto na kuweka mikakati ya kukabiliana nazo ili kuongeza tija na mchango wa ushirika katika maendeleo ya wananchi.

Mgeni rasmi katika ufunguzi wa jukwaa hilo alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Dunstan Kyobya, ambaye amemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mheshimiwa Adam Malima.
Akijibu hoja na changamoto zilizowasilishwa, Wakili Dunstan Kyobya amesisitiza umuhimu wa kuzingatia weledi, uadilifu, uwazi na ushirikishwaji katika utoaji wa huduma kwa wanachama wa vyama vya ushirika huku akitaka viongozi na watendaji wa ushirika kuchukua hatua madhubuti za kuzuia vitendo vya rushwa ili kuongeza ufanisi katika utendaji na kuimarisha imani ya wanachama.
Aidha, Kyobya amesema Serikali imezipokea changamoto zilizowasilishwa na yuko tayari kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuzitafutia ufumbuzi kwa kushirikiana na wakuu wa wilaya zingine ndani ya Mkoa wa Morogoro katika kushughulikia baadhi ya changamoto za pamoja, ikiwemo migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji ambayo imekuwa ikiathiri shughuli za uzalishaji na maendeleo ya ushirika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Grace Masambaji, amesema baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika vyama vya ushirika zinatokana na utendaji wa viongozi wenyewe, hivyo ni muhimu viongozi hao wawajibike kwa matendo yao na kuzingatia misingi ya utawala bora katika usimamizi wa vyama wanavyoongoza.

Jukwaa hilo linalofanyika chini ya kauli mbiu isemayo “Ushirika kwa dunia yenye amani: linda ushirika, chagua uadilifu.” linatarajiwa kutoa fursa kwa washiriki kubadilishana uzoefu, kujadili mbinu bora za kuimarisha ushirika na kuweka mikakati ya pamoja itakayochochea maendeleo ya sekta hiyo katika Mkoa wa Morogoro na nchini kwa ujumla.