Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
6 June 2025, 16:42

Tusikimbie majukumu yetu tusipowafuatilia na kuwasimamia vizuri ndio tunapata Wezi wa Mtandaoni(halo halo)muda mwingine hamkagui daftari kwa sababu tumeshindwa kutimiza wajibu wetu
Na Katalina Liombechi
Wazazi wametakiwa kuwajibika kwa watoto wao kufanikisha maendeleo ya kitaaluma na Malezi ili kukuza ufaulu na kuchochea maendeleo yao katika ukuaji.
Afisa Mtendaji Mtaa wa Mhola Ally Bungala akizungumza katika kikao cha wazazi katika Shule ya Msingi Ifakara kwa niaba ya Mtendaji wa Kata hiyo Bi Hawa Ndachuwa amesema ni lazima wazazi kuwajibika kusimamia malezi ya watoto wao kwa mahitaji yote na kufuatilia nyendo zao ili kujiridhisha kama wanahudhuria shuleni ipasavyo na hawajihusishi na tabia zisizofaa.
Amesema wazazi wanoposhindwa kwenye malezi na kuwafuatilia watoto wao inapelekea uwepo wa vijana wanaojihusisha na wizi wa Mtandaoni na kuibuka kwa wadada wanaojiuza tabia ambazo amesema hazina tija kwa Taifa huku akikemea tabia ya wazazi wanaohamia mashambani na kuwaacha watoto bila ya uangalizi.

Akizungumzia suala la lishe shuleni hapo Mwalimu Mkuu Bi Esther Nuruva amesema kumekuwa na uchangiaji hafifu wa lishe ukilinganisha na siku za nyuma hali inayochangia utoro hivyo kuhatarisha kushuka kwa ufaulu jambo ambalo amewasisitiza wazazi kulichukulia umuhimu kama walivyokubaliana katika vikao vya nyuma kuchangia kiasi cha Shilingi 3000/= kila mwezi kwa ajili ya uji ili walimu watekeleze majukumu yao kikamilifu.

Mmoja wa Wazazi akizungumza katika kikao hicho ameeleza kuunga mkono suala la lishe huku akitaka uangalizi wa watoto na kuzingatia hali ya usafi muda wanaokunywa uji ili kuzuia magonjwa yatokanayo na uchafu.