Pambazuko FM Radio

Ifakara kuendelea kukamilisha maboma ya kata

17 August 2026, 16:21

Baadhi ya madiwani wa halmashauri ya mji wa Ifakara – picha na: Jackline Jerome

Halmashauri ya Mji wa Ifakara imeeleza kuwa itakamilisha maboma ya kata na vijiji hatua kwa hatua kadri bajeti itakavyopatikana, kufuatia ombi la Diwani wa Kisawasawa, Justus Ndege. Katika kikao hicho cha Baraza la Madiwani, Mwenyekiti Kassim Nakapala aliwataka viongozi kusimamia bajeti vizuri, huku baraza likiipongeza halmashauri kwa kushika nafasi ya pili kwenye Maonesho ya Wakulima 2026 Kanda ya Mashariki.

Halmashauri ya Mji wa Ifakara wilayani Kilombero inaendelea na mkakati wa kukamilisha maboma ya ofisi za vijiji na kata ambayo bado hayajakamilika. Akijibu swali lililoulizwa na Diwani wa Kata ya Kisawasawa katika Kikao cha Nne cha Baraza la Madiwani, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Rashid Semgoya, amesema kuwa ujenzi na ukamilishaji huo utafanyika hatua kwa hatua kadri ya upatikanaji wa rasilimali na bajeti.

Sauti ya Rashidi Semgoya

Awali, Diwani wa Kata ya Kisawasawa, Justus Ndege, aliihoji halmashauri hiyo kuhusu kutokamilika kwa boma la ofisi ya kata tangu mwaka 2009, huku akiomba kata hiyo kupewa kipaumbele maalumu kwa kuwa ni miongoni mwa kata kongwe zaidi katika eneo hilo.

Diwani wa kata ya Kisawasawa, Justin Ndege – picha na: Jackline Jerome
Sauti ya Diwani wa Kisawasawa

Akizungumzia suala la bajeti, Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Ifakara Mji, Kassim Nakapala, amewasihi madiwani wenzake kuzingatia na kusimamia kwa uaminifu mipango yote iliyopitishwa kwenye bajeti ya halmashauri ili kuchochea maendeleo.

Kassim Nakapala (mwenyekiti wa baraza la madiwani Ifakara mji) – picha na: Jackline Jerome
Sauti ya Kassim Nakapala

Katika hatua nyingine, kikao hicho kilipata fursa ya kuipongeza halmashauri hiyo kwa kufanya vizuri na kuibuka washindi wa nafasi ya pili katika Maonesho ya Wakulima (Nane Nane) ya mwaka 2026 kwa Kanda ya Mashariki.