Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
11 September 2026, 13:12

Baraza la ushauri la wazee mkoa wa Morogoro limeitaka serikali na halmashauri kuongeza ushirikishwaji wa wazee katika vyombo vya maamuzi, likisema ushiriki wao bado haujawa wa kutosha. Serikali kwa upande wake imeahidi kuhakikisha wazee wanapata uwakilishi katika vikao vya maamuzi kuanzia ngazi ya kijiji na mtaa hadi mkoa, huku ikieleza kuwa Mkoa unakabiliwa na upungufu wa Maafisa Ustawi wa Jamii.
Na; Isidory Mtunda
Baraza la ushauri la wazee mkoa wa Morogoro limeitaka serikali na halmashauri kuongeza ushirikishwaji wa wazee katika vyombo vya maamuzi, likisema kundi hilo lina uzoefu na mchango muhimu katika maendeleo ya jamii.
Baraza hilo limesema ushiriki wa wazee katika vikao vya maamuzi bado haujawa wa kutosha, licha ya kuwepo kwa mabaraza ya wazee kuanzia ngazi ya vijiji na mitaa hadi taifa, amesema Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la wazee mkoa wa Morogoro, mzee Samweli Mpeka.

Ikijibu maombi hayo, Serikali imeeleza kuwa wazee wanapaswa kuwa na wawakilishi katika vikao mbalimbali vya maamuzi kuanzia ngazi ya kijiji, mtaa, kata, wilaya hadi mkoa.
Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa wilaya ya Kilombero, wakili Dunstan Kyobya, aliyekuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Morogoro, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga

Wakati huo huo, mkuu huyo wa wilaya amesema mkoa unatambua changamoto ya upungufu wa Maafisa Ustawi wa Jamii, ambapo kwa sasa wapo watumishi 85 sawa na asilimia 26 ya mahitaji ya watumishi 329, na kwamba hatua zimeanza kuchukuliwa ili kuimarisha upatikanaji wa watumishi hao.