Pambazuko FM Radio

Polisi wapiga marufuku abiria wengi

10 August 2026, 12:45

wamiliki na madereva wa Boda boda na Bajaji wakipatiwa mafunzo Tarafa ya Ifakara – picha na Kuruthum Mkata

Jeshi la Polisi Wilaya ya Kilombero limewataka madereva wa bodaboda, bajaji na guta kuzingatia sheria za usalama barabarani, ikiwemo kutobeba abiria zaidi ya mmoja kwa bodaboda na bajaji, huku guta likisisitizwa kuwa chombo cha kubeba mizigo.

Na; Kuruthum Mkata

Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kilombero (OCD), SP Diventine Nyahoro, amepiga marufuku matumizi ya vyombo vya moto, ikiwemo bodaboda na bajaji, kubeba abiria zaidi ya mmoja, huku akisisitiza kuwa guta ni chombo cha kubeba mizigo na si abiria.

OCD Kilombero SP Diventine Nyahoro – picha na: Kuruthum Mkata

Akizungumza wakati wa kufungua kikao cha madereva wa bajaji, bodaboda na guta wilayani Kilombero, OCD SP Nyahoro amesema hatua hiyo inalenga kuimarisha usalama wa watumiaji wa barabara. Amewataka wamiliki wa vyombo hivyo kuhakikisha madereva wanaowaajiri wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani.

sauti ya OCD – SP Nyahoro

Kwa upande wake, Mkuu wa Usalama Barabarani Wilaya ya Kilombero, DTO ASP Blandina Kasongwa, amewataka madereva kuhakikisha vyombo wanavyoviendesha vimesajiliwa na vina nyaraka halali, huku madereva wakiwa na leseni zinazotambulika kisheria. Amesisitiza kuwa uzingatiaji wa sheria za usalama barabarani ni muhimu katika kupunguza ajali.

DTO ASP Blandina Kasongwa akitoa maelekezo kwa wamiliki na madereva wa Boda boda na Bajaji – picha na; Kuruthum Mkata
Sauti ya DTO ASP B Kasongwa

Naye Ofisa Mfawidhi wa LATRA Ifakara, Amani Mwakalebela, amesema viwango vipya vya tozo vilianza kutumika Julai mwaka huu, ambapo tozo kwa bodaboda imeongezeka kutoka shilingi 17,000 hadi 22,000, huku bajaji ikiongezeka kutoka shilingi 22,000 hadi 32,000.

Afisa mfawidhi LATRA Amani Mwakalebela – picha na; Kuruthum Mkata
Baadhi ya madereva na wamiliki wa vyombo vya moto waliohudhuria kikao hicho wameishukuru Jeshi la Polisi kwa kutoa elimu ya usalama barabarani, huku wakieleza changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika shughuli zao na kuomba mamlaka husika kuendelea kuwapatia elimu na kuwaelekeza kuhusu utekelezaji wa sheria.
Sauti za wamiliki na madereva wa Boda boda na Bajaji