Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
29 May 2026, 10:44

STEP kupitia ufadhili wa Polish aid wanalenga kuendeleza ufugaji bora wa kuku wa kienyeji kama njia muhimu ya kuongeza kipato cha familia na jamii
Na Katalina Liombechi
Shirika linalojihusisha na uhifadhi wa tembo kusini mwa Tanzania,Southern Tanzania Elephant Program (STEP) kupitia ufadhili wa Polish Aid, limeendelea kuvijengea uwezo vikundi mbalimbali katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara kwa kutoa mafunzo ya ufugaji kuku wa kienyeji.
Mafunzo hayo yamejikita katika afya ya kuku pamoja na namna ya kukabiliana na magonjwa yanayoathiri mifugo hiyo.
Akizungumza Mei 28, 2026 katika Kata ya Lumemo, Mratibu wa Mahusiano na maisha endelevu kutoka STEP, Catherine Kimario, amesema mafunzo hayo yameandaliwa baada ya kubaini kuwa ufugaji wa kuku wa kienyeji una mchango mkubwa katika kuongeza kipato kwa wananchi.
Amesema elimu hiyo itasaidia wananchi kufuga kisasa zaidi, kuongeza kipato na kupunguza utegemezi wa shughuli moja ya kilimo pamoja na kuzuia vitendo vya uharibifu wa mazingira katika maeneo ya hifadhi.

Vikundi vilivyonufaika na mafunzo hayo ambayo katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara yalizinduliwa mei 25,2026 ni pamoja na Tunza Mazingira na Misitu ni Hazina kutoka kata ya Lumemo, Wahifadhi Machipi kuta ya Michenga pamoja na Tuwarithishe kutoka Signali.
Kwa upande wake, Afisa Mifugo kutoka kampuni ya NIR Animal Trust ya Arusha, James Julius, amesema wafugaji wengi wa kuku wa kienyeji bado hawazingatii kanuni bora za ufugaji hali inayochangia kuenea kwa magonjwa.
Amesema ugonjwa wa Kideri ni miongoni mwa magonjwa hatari kwa kuku na njia bora ya kuudhibiti ni kutoa chanjo kwa wakati kabla kuku hawajaugua.

Naye Daktari wa Mifugo wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara Dkt.Dunia Mlanzi amewataka wananchi kuendeleza ufugaji bora wa kuku kwa kuwa ni njia muhimu ya kuongeza kipato cha familia huku akieleza kuheshimu mchango wa wadau kama STEP kupitia Polish aid kuisaidia serikali kuendeleza sekta ya mifugo ili kuinua uchumi wa wananchi.

Baadhi ya wanufaika wa mafunzo hayo kikundi cha Tunza Mazingira Lumemo wameishukuru STEP pamoja na Polish Aid wameelezea uzoefu wao katika ufugaji wa kuku wa kienyeji huku wakisema elimu waliyoipata itasaidia kuboresha maisha yao kupitia ufugaji wa kuku wa kienyeji.

Tangu mwaka 2014, STEP imekuwa ikitekeleza shughuli za uhifadhi wa tembo, mazingira na utoaji wa elimu ya uhifadhi kwa jamii na kuwezesha njia mbadala ya kipato katika maeneo mbalimbali kusini mwa Tanzania .