Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
8 June 2026, 13:06

Uwepo wa madaktari hao ni fursa muhimu kwa wananchi kupata huduma za kibingwa karibu na maeneo yao, huku pia ikichangia kubadilishana uzoefu na ujuzi wa kitabibu
Na Katalina Liombechi
Wananchi wa Ifakara na maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro wamehimizwa kutumia fursa ya kupata matibabu ya kibingwa yanayotolewa bure na madaktari bingwa kutoka Italia walioweka kambi katika Hospitali ya Rufaa ya St. Francis kwa kipindi cha wiki mbili kuanzia leo, Juni 8, 2026.
Akizungumza kuhusu huduma hizo, Mkurugenzi wa Tiba wa hospitali hiyo, Daktari Winifrid Gingo, amesema madaktari hao watatoa huduma mbalimbali za kibingwa ikiwemo matibabu ya magonjwa ya pua, sikio na koo,Goita, upasuaji wa kurekebisha makovu yatokanayo na moto na ajali.

Mengine ni Vidonda sugu,kuondoa vimbe kwenye matiti, matibabu ya magonjwa ya ngozi,upimaji wa saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake pamoja na matibabu ya jumla huduma ambazo zitatolewa bure.
Daktari Gingo amesema uwepo wa madaktari hao ni fursa muhimu kwa wananchi kupata huduma za kibingwa karibu na maeneo yao, huku pia ikichangia kubadilishana uzoefu na ujuzi wa kitabibu kati ya wataalamu wa afya wa Hospitali hiyo na wenzao kutoka Italia.
Ametoa wito kwa wananchi wenye changamoto za kiafya zinazohusiana na huduma hizo kujitokeza kwa wingi ili kunufaika na matibabu hayo ndani ya kipindi chote cha kambi hiyo.

Baadhi ya wananchi waliojitokeza kupata huduma hizo wameeleza kuridhishwa na namna walivyopokelewa hospitalini hapo, wakisema wana matumaini ya kupata nafuu na kuondokana na magonjwa yaliyokuwa yakiwasumbua kwa muda mrefu.
