Pambazuko FM Radio

DC Kyobya ataka ufugaji kuku wenye tija

27 April 2026, 19:29

Picha ya DC Kyobya (katikati) akizindua mafunzo ya ufugaji kuku Ifakara(Picha na Kuruthumu Mkata)

Akizindua mafunzo ya ufugaji wa kuku bora Mkuu wa Wilaya amewagiza wataalamu kuhakikisha wanawatembelea wafugaji mara kwa mara ili kuwapa ushauri wa kitaalamu pamoja na kuwawezesha kupata mikopo

Na Kuruthumu Mkata

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Dunstan Kyobya, leo Aprili 27, 2026, amezindua rasmi mafunzo ya ufugaji bora na salama wa kuku, akisisitiza umuhimu wa wananchi kuwekeza katika ufugaji wenye tija huku wakizingatia viwango vya usalama.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Kyobya amewahimiza wananchi wa Kilombero kujikita katika ufugaji wa kisasa wa kuku ili kuongeza kipato na kuboresha maisha yao.

Aidha, ameagiza maafisa maendeleo kuhakikisha wanawatembelea wafugaji mara kwa mara ili kuwapa ushauri wa kitaalamu pamoja na kuwawezesha kupata mikopo kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao.

Katika hatua nyingine, Kyobya amesisitiza umuhimu wa wafugaji kuunda umoja wao, akieleza kuwa hatua hiyo itarahisisha upatikanaji wa huduma, mikopo na masoko huku akiwapongeza KV HELP waandaaji wa Mafunzo hayo kwa juhudi zao za kuwapa mbinu wananchi ya kujikwamua kiuchumi.

Picha ya DC Kyobya akihutubia kwenye ufunguzi mafunzo ya ufugaji kuku(Picha na Kuruthumu Mkata)
Sauti ya DC Kyobya

Kwa upande wake, mratibu wa mafunzo hayo yanayofanyika kwa siku nne kuanzia leo Aprili 27,2026 Katika Ukumbi wa vijana Halmashauri ya Mji wa Ifakara Idd Mayumana kutoka KV HELP, amesema wafugaji wengi wamekuwa wakipata hasara kutokana na ukosefu wa elimu sahihi ya ufugaji, hasa katika matumizi ya dawa akieleza kuwa matumizi ya dawa yasiyo sahii husababisha vifo vya kuku na kupunguza uzalishaji.

Picha ya Idd Mayumana Mratibu KV HELP(Picha na Kuruthumu Mkata)
Sauti ya Idd Mayumana Mratibu KV HELP

Naye Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara, Bi Florence Mwambene, amewahimiza wafugaji kutumia fursa za mikopo zinazotolewa na taasisi mbalimbali ili kuongeza mitaji na kuboresha ufugaji wao.

Sauti ya Bi Florence Mwambene Afisa Maendeleo

Hata hivyo, baadhi ya wafugaji walioshiriki mafunzo hayo wameiomba serikali kuhakikisha upatikanaji wa soko la uhakika kwani kwa sasa wanakabiliwa na changamoto ya masoko, hali inayowalazimu kuuza kuku kwa bei ya chini kupitia wauzaji wa kati na pembezoni mwa barabara.

Picha ya washiriki wa mafunzo(Picha na Kuruthumu Mkata)
Sauti za wananchi walioshririki mafunzo