Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
14 May 2026, 20:53

Mradi wa FOLUR unaendelea kuleta matokeo chanya kwa kuunganisha uhifadhi wa mazingira na uzalishaji endelevu
Na Katalina Liombechi
Hifadhi ya Mazingira Asili Uzungwa Scarp imepanda zaidi ya miti elfu nane ya Mikangazi na Mikenge katika safu ya Chita, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa Urejeshaji wa Mifumo ya Chakula, maarufu FOLUR.
Mradi huo unalenga kurejesha uoto wa asili, kulinda vyanzo vya maji, kuhifadhi bioanuwai pamoja na kuhamasisha matumizi endelevu ya rasilimali za mazingira.
Mhifadhi daraja la kwanza kutoka hifadhi hiyo, Maiko Urio, amesema mradi huo unaendelea kuleta matokeo chanya kwa kuunganisha uhifadhi wa mazingira na uzalishaji endelevu wa chakula kwa manufaa ya jamii na vizazi vijavyo.
Katika hatua nyingine kupitia Mradi huo wa FOLUR Hifadhi ya Mazingira Asili Uzungwa Scarp pia wametoa mafunzo ya kukabiliana na mioto ya misituni kwa zaidi ya wananchi mia mbili kutoka vijiji vinane vinavyozunguka hifadhi hiyo amnapo kwa Safu ya Chita ni vijiji vya Udagaji,lufulu,Ching’anda,Chita,Makutano,Ikule,Kidete na itongoa.
Aidha pamoja na mambo mengine Mhifadhi Maiko ameelezea umuhimu wa hifadhi hiyo kiikolojia na tija iliyopo kwa shughuli za utalii na matumizi mengine endelevu.
Kwa upande wake miongoni mwa wawezeshaji wa mafunzo hayo, Arafat Mtui, amesema elimu hiyo inalenga kuwajengea wananchi uwezo wa kuzuia moto na kushiriki katika kulinda mazingira.

Mioto ya misituni imekuwa ikisababisha uharibifu mkubwa wa bioanuwai, vyanzo vya maji na makazi ya viumbe mbalimbali. Kupitia mafunzo haya tunahamasisha ushirikiano kati ya wananchi na wahifadhi katika kulinda mazingira yetu
Mradi wa FOLUR unatekelezwa kwa miaka mitano kwa ufadhili wa Mfuko wa Mazingira Duniani, ambapo katika Tanzania Bara unatekelezwa katika Halmashauri ya Mlimba kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni sita.