Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
7 September 2026, 21:16

Na: Henry Mwakifuna
Wadau wanaojihusisha na shughuli za bidhaa za misitu Wilayani Kilombero, Mkoa wa Morogoro, wametakiwa kufuata utaratibu wa kujisajili na kuzingatia sheria na kanuni zinazosimamia shughuli hizo.
Akizungumza na Redio Pambazuko FM, Mhifadhi kutoka Wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS), Kilombero CR2, Nhandi Petro, amesema mwisho wa muda wa usajili kwa wadau hao ni Septemba 30, 2026.
Mhifadhi Nhandi amesema baada ya muda huo kumalizika, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaobainika kuendelea kufanya shughuli za bidhaa za misitu bila kufuata matakwa ya sheria.
Ameeleza kuwa mtu atakayekiuka sheria anaweza kukabiliwa na faini ya hadi shilingi milioni moja, kifungo kisichozidi miaka miwili, au adhabu zote mbili kwa pamoja, kulingana na matakwa ya sheria husika.

TFS imewataka wadau wanaohusika na bidhaa za misitu kuhakikisha wanatumia kipindi kilichobaki kukamilisha taratibu za usajili na kufanya shughuli zao kwa mujibu wa sheria.