Pangani FM
Pangani FM
6 June 2024, 10:43

Kila mwaka katika miezi mitatu kuanzia Aprili wilaya ya Pangani imekuwa ikiandikisha ajali kadhaa za baharini zinazochukua makumi ya wakazi wa wilaya hiyo.
Na Hamisi Mkungu
Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la AWESO SALIM MOHAMMED maarufu Aweso Rungo amefariki akiendelea na shughuli za uvuvi katika Bahari ya Hindi eneo la Mhembo lililopo Wilayani Pangani.
Mvuvi huyo anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 50 hadi 52 amefariki jumatano asubuhi akiwa ndani ya maji baada ya kuzidiwa na nguvu ya maji, ambapo kabla ya kufikwa na umauti alipiga kelele za kuomba msaada.
Akithibitisha tukio hilo Mwenyekiti wa Kijiji cha Pangani Mashariki Rajabu Kitwana Nyembo amesema tukio hilo ni la pili kutokea ndani ya mwaka huu.
Akisimulia mkasa huo shuhuda wa tukio hilo Ali Abdala Mshauri amesema asubuhi wakiwa ndani ya maji kuendelea na shughuli za uvuvi, hali ya mwenzake ilibadilika hafla ambapo jitihada za kujaribu kuokoa Maisha yake zilishindikana.
Mganga Mfawidhi katika Hospitali ya Wilaya ya Pangani Dokta Hassan Msafiri amethibitisha kupokea mwili huo majira ya asubuhi na kwamba taratibu za kuukabidhi mwili huo kwa familia zinaendelea.
Mwezi wa tatu Mwaka huu mvuvi mmoja alifariki katika eneo la Muhembo wakati akiendelea na shughuli za uvuvi, kama anayoeleza Mzee Abdallah Mshauri Ramadhani mvuvi wa samaki aina ya Makaji aliyeshuhudia tukio hilo.
Pangani FM inatoa pole kwa ndugu, jamaa na wote walioguswa na msiba huo. SISI NI WA MUNGU, NA KWAKE TUTAREJEA.
AMIN.