Sibuka FM
Sibuka FM
30 July 2026, 17:15

“Tunahitaji kuona kundi la vijana wanajisimamia wao kiuchumi na siyo kuanza kulaumu serikali kwamba haitoi ajira wakati tayari serikali kupitia halmashauri kuna asilimia kumi ya mapato ya ndani inawasubiri wao ili kujikwamua kiuchumi kupitia vikundi”.
Na,Daniel Manyanga
Mkuu wa wilaya ya Bariadi mkoni Simiyu, Simon Simalenga amewataka maafisa maendeleo ya jamii kuanzia ngazi ya kata na halmashauri kuhakikisha wanatoa elimu kwa vijana ili wachangamkie fursa mbalimbali zilizopo katika wilaya hiyo ambazo zinaweza kusaidia kundi hilo kujikwamua kiuchumi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa jukwaa la vijana katika halmashauri ya mji wa Bariadi,Simon Simalenga amesema kuwa wilaya hiyo inazo fursa mbalimbali ambazo zinaweza kuwanufaisha vijana hivyo ni muhimu kutolea kwa elimu na umuhimu wa fursa hizo.
Iddi Ndabhona ni mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji wa Bariadi amesema kuwa halmashauri hiyo inaendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuwafikia vijana na kuwaelimisha ili waunde vikundi vitakavyowawezesha kupata mikopo inayotolewa na halmashauri kupitia mapato yake ya ndani.
Baadhi ya vijana wenye ulemvu akiwemo Enock John, Krypton Mmanga na Alex Mwaisumo wameiomba serikali kuongeza ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu kwenye fursa mbalimbali na kwamba hata wao wanaweza kutoa mchango wenye tija kwenye jamii.