Sibuka FM
Sibuka FM
9 September 2024, 17:48

“Uboreshaji wa taarifa katika daftari la kudumu la wapiga kura ndiyo dira halisi na mwanzo wa kupata viongozi bora wanaochaguliwa na wananchi kwa maendeleo ya Taifa letu hivyo hatuwezi kuvumilia vitendo vya kuvuruga zoezi hilo”.
Na, Daniel Manyanga
Ikiwa leo imesalia siku moja pekee kabla ya kuhitimishwa kwa zoezi la uboreshaji wa taarifa katika daftari la kudumu la wapiga kura mkoani Simiyu, wananchi katika jimbo la Kisesa wilayani Meatu mkoani humo wameshindwa kushiriki kikamilifu katika zoezi hilo kutokana na kamata kamata katika operesheni inayofanywa katika jimbo hilo kwa watu wasiozingatia sheria za usafi wa mazingira ikiwemo matumizi sahihi ya vyoo.
Wakizungumza mbele ya mbunge wa jimbo hilo, Luhaga Mpina katika ziara aliyoifanya kwa ajili ya kutembelea vituo vya uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura katika kata za Nzanza, Mwabusalu na Tindabuligi, wananchi hao wameeleza namna ambavyo wamekwamishwa kushiriki katika zoezi hilo baada ya kuyakimbia makazi yao wakihofia kukamatwa.

Baada ya kusikiliza malalamiko ya wananchi hao mbunge wa jimbo la Kisesa Luhaga Mpina, akatoa siku saba wananchi hao warejeshewe pesa zao walizotozwa faini kama faini ya kutokutii matumizi sahihi ya vyoo na usafi wa mazingira.
Aidha Mpina ameeleza hatua atakazozichukua ili kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ili waweze kuwa na sifa za kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu hapo mwakani.
Akizungumza na Sibuka Fm kwa njia ya simu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Meatu ,Athman Masasi ametoa ufafanuzi juu ya operesheni hiyo ambayo ameeleza kuwa haikulenga kumuonea mtu yeyote hivyo haiingiliani na zoezi la uboreshaji wa taarifa katika daftari la kudumu la wapiga kura.

