Sibuka FM
Sibuka FM
8 August 2024, 21:54

Na Nicholaus Machunda – Simiyu
Wananchi wa Mikoa ya Shinyanga , Simiyu na Mara wameaswa kutumia teknolojia ya kisasa ya kilimo ili kujikwamua kiuchumi kwa kuongeza uzalishaji.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe, Kanali Evans Alfred Mtambi ambaye alikuwa Mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya Sikukuu ya Wakulima maarufu kama Nanenane.
Aidha Mh. Mtambi amewaagiza Makatibu Tawala wa Mikoa mitatu inayounda Kanda ya Ziwa Mashariki kukutana mara moja ili kuanza mipango ya kuandaa miundombinu ya msimu ujao ili kuwe na Maonyesho yenye tija kwa Wakulima na wafugaji.
Akimkaribisha Mgeni rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu ambaye ndio mwenyeji wa Maadhimisho hayo Mhe, Kenani Laban Kihongosi amesema kuwa ifike wakati wakulima wabadilike katika kutumia mbinu na Zana Bora za kilimo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe, Anamringi Macha amewataka wakulima na Wafugaji mikoa ya Kanda ya ziwa Mashariki (Mara, Simiyu na Shinyanga ) waendelee kuja katika viwanja vya Nyakabindi ili kunifunza zaidi.
Akitoa salamu za Chama, mwenyekiti wa chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mara Ndg. Patrick Chande Marwa amewapongeza wandaaji wa sherehe hizo na kuwaomba waongeze ubunifu ili mwakani yafae zaidi.
Kauli mbiu katika sherehe za Wakulima Nane nane kwa mwaka huu 2024 ni Chagua Viongozi Bora wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
