Sibuka FM
Sibuka FM
11 November 2025, 11:23

“Hakuna maendeleo ya vitu bila watu ndiyo maana sasa duniani kote wanapambana sana kuleta ustawi wa afya za watu wakijuwa kabisa kwamba watu wakiwa na afya imara hata uchumi nao utakuwa kwa kasi kwa sababu tu wananchi wake wako na afya na nguvu kufanya kazi za kiuchumi”.
Na, Daniel Manyanga
Mkuu wa wilaya ya Maswa mkoani Simiyu nchini Tanzania, Dkt. Vicent Naano Anney amewataka watumishi wa kituo cha afya cha Barikiwa mjini Maswa kinachomilikiwa na mzawa wa mjini hapo, Dkt. Ashrey Lucas kufanya kazi kwa weledi katika kuwahudumia wananchi wanaokuja kupata huduma mbalimbali za matibabu kituoni hapo.

Dkt. Anney amesema hayo wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi katika jengo la X-Ray katika kituo hicho ili kuongeza upatikanaji wa huduma muhimu za matibabu kwa wananchi pamoja na kupunguza gharama za kufuata huduma hiyo sehemu nyingine.

Kwa upande wake mkurugenzi wa kituo cha afya cha Barikiwa ,Dkt.Ashrey Lucas amesema kuwa wataendelea kuleta madaktari bingwa kutoka hospitali mbalimbali hapa nchini katika kutoa huduma za kibingwa huku mganga mkuu wa wilaya ya Maswa, Dkt. Hadija Zegega amemshukuru Dkt. Ashrey kwa uwekezaji huo ambao unasaidia wananchi kupata huduma bora za matibabu kwa ushirikiano na serikali.

Jamali Mtende na Bertha Machama ni baadhi ya wanufaikaji wa kituo hicho cha afya waliopatiwa matibabu wameshukuru kwa namna ambavyo kituo hicho kinavyotoa huduma za kibingwa kwa nyakati tofauti hivyo kuwapunguzia adha ya kufuata huduma hizo sehemu zingine.

