Boma Hai FM
Boma Hai FM
12 September 2026, 6:44 am

Chama cha Akiba na Mikopo cha HRT Saccos kimeendelea kutoa elimu na mafunzo kwa wanachama wake kuhusu matumizi ya teknolojia kwa lengo lakutoa huduma kwa urahisi na usahihi pamoja na kuendana na kasi ya sayansi na teknolojia kwenye vyama vya ushirika.
Na Henry Keto, Hai-Kilimanjaro
Wanachama wa chama Cha Akiba na Mikopo Cha HAI RURAL TEACHERS SACCOS wameaswa kutumia teknolojia kwenye shughuli za chama kuongeza ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wanachama wa HRT SACCOS.
Wito huo umetolewa Septemba 11,2026 wakati wa Mkutano wa dondoo kwa Wanachama wa Tarafa za Lyamungo na Machame wenye lengo la Wanachama kujua maendeleo ya chama, pamoja na kutoa maoni yao kuelekea mkutano mkuu wa Chama unaotarajiwa kufanyika Novemba 7, 2026.
Afisa Tehama wa HRT SACCOS Emmanuel Bura ameeleza sababu za chama kutumia teknolojia, lengo ikiwa ni kurahisisha majukumu ya kazi kwa kupunguza Changamoto kwa Wanachama kufika ofisini ili kuhudumiwa kutokana na umbali kutoka majumbani Hadi ofisini na kupunguza msongamano kwa wanachama kusubiri huduma muda mrefu.

Nae Meneja wa HRT SACCOS, Upendo Lyatuu amehimiza matumizi ya teknolojia kwa wanachama akiwataka kuendana na mifumo ya kisasa huku akieleza faida za mafunzo yaliyotolewa kwa wanachama kuhusu afya ya akili, bidhaa na huduma zinazotolewa na Chama kwa kuzingatia Masharti ya Chama, sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia Vyama vya Ushirika Tanzania.

Nao wanachama walioshiriki Mkutano huo, wameshukuru uongozi wa chama kwa kuona umuhimu wa kuwaletea mafunzo ya afya ya akili kwa sababu ni tatizo kubwa kwasasa kwa wafanyakazi wengi, lakini pia kuwapa Elimu ya teknolojia katika kupata huduma, Pamoja na kupata taarifa za Chama. Wametoa wito kwa Wanachama wote kuendelea kushirikiana na kukitumia chama Cha HRT SACCOS kwani kina manufaa makubwa.