Boma Hai FM

Ushirika Hai waanza kuleta tija, Saashisha aishukuru serikali

13 March 2024, 12:13 pm

Mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe (katikati)akishuhudia makabidhiano ya mkataba wa wazi kati ya mwenyekiti wa Muroso Usangi pamoja na mwekezaji wa kampuni ya Macjaro mara baada ya utiaji saini wa mkataba huo(picha na Edwin Lamtey)

Mkataba wa kwanza wa wazi wasainiwa kati ya chama cha ushirika cha Muroso Sangi na kampuni ya Macjaro watajwa kuwa mkataba wenye tija kwa wananchi.

Na Edwin Lamtey

Mkataba wa kwanza wa Wazi katika vyama vya ushirika na ulioandikwa kwa lugha ya kiswahili na kingereza umesainiwa leo kati ya chama cha ushirika cha MUROSO SANGI dhidi ya Kampuni ya MACJARO LTD ambapo unatajwa kuwa ni mkataba wenye manufaa zaidi baada ya kuwa na mashirikiano baina ya pande zote mbili.

Akizungumza wakati wa utiliaji saini katika mkataba huo mwenyekiti wa bodi ya ushirika wa Muroso Sangi Bw. Alex Kimaro amesema kuwa matumizi ya lugha ambayo inaeleweka kwa ufasaha na wajumbe wote pamoja na uwazi uliopo katika mkataba huo vimesaidia kujenga uwazi kwa wanachama na wananchi kwa ujumla huku matarajio yake yakionekana kuwanufaisha wananchi pamoja na pande zote za mkataba.

“Nikushukuru sana mbunge wetu Saashisha kwa kuyapambania haya mambo ya ushirika, leo tunasaini mkataba huu wazi tena hakuna kificho na hata ukimsimamisha mjumbe yeyote wa bodi anajua bei halisi ya ukodishwaji pamoja na mgao wote jambo ambalo kwa miaka yote katika vyama vyetu lilikuwa ni siri”. Alisema Kimaro

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe ambaye ameshuhudia utiaji saini huo ameishukuru serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt Samia Suluhu hasani kwa kuzifanyia kazi changamoto za ushirika ikiwemo ile ya mikataba mibovu na ambayo haikuwa na uwazi jambo ambalo lilipelekea vyama vingi vya ushirika kuonekana kutokuwa na tija kwa jamii.

“Leo ninayofuraha kubwa moyoni mwangu na leo historia imeandika mkataba mpya na wawazi, mkataba wenye mambo mengi mazuri ikiwemo ushirikishwaji, mpango wa maendeleo ya shamba, mpango wa ujenzi wa viwanda viwili pamoja na uwepo wa namna nzuri ya kupeleka fedha kwenye kijiji” Alisema Saashisha.

“Naondoka  hapa na furaha nikujua ushirika wa hapa undenda kutoa ajira, vijiji vinakwenda kunufaika na sasa nauona ushirika wa wilaya ya Hai unaimarika kwa kiwango kikubwa tofauti na ilivyokuwa hapo awali”.

Aidha amesema kuwa kusainiwa kwa mkataba huo kumeonesha mwanga mzuri wa matumaini katika vyama vingine na kuwaasa viongozi wake kushirikiana na kutambua kuwa mashamba yanayomilikiwa na ushirika sio mali ya mtu binafsi bali ni mali ya umma.

Sauti ya Mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe.

Katika zoezi hilo la utiaji saini wa mkataba huo, lilihudhuriwa pia na mrajisi wa vyama vya Ushirika nchini Bw. Benson Ndiege ambaye amesema kuwa mabadiliko makubwa yanayoonekana katika vyama vya ushirika yanatokana na ushirikiano mzuri wa mbunge Saashisha huku pia akiwataka viongozi wa vyama vya ushirika kutambua kuwa viongozi wanaotokana na kuchaguliwa wanapaswa kushirikishwa na kuyafahamu yale yanayoendelea ndani ya vyama hivyo.

“Ni kweli hii ni hatua nzuri kwa vyama vyetu, nayaona yale yaliyokuwa yanahojiwa na mbunge pale bungeni na hata alipofika ofisini kwetu, mbunge, diwani, mwenyekiti na hata mkuu wa wilaya wapo kwaajili ya kuwawakulisha wananchi kutoka katika maeneo yao na mnaposema hawaruhusiwi kujua yanayoendelea sio sahihi, waalikeni waje watoe michango yao pale kwenye maamuzi ya wanachama mfano mambo ya kura ninyi mtaendelea na taratibu zenu maana wasiposemea wananchi wao nani atawasemea? Mbona mkigombana mnakimbilia kwa Dc ni kwasababu mnajua mamlaka yake ya kuwasaidia”. Alisema Benson – Mrajisi wa vyama vya ushirika nchini.

Nae mwekezaji wa kampuni hiyo ya MACJARO LTD ameishukuru serikali wilayani Hai kwa kuweka mazingira bora ya uwekezaji huku akidai kuwa shughuli ramsi zitaanza rasmi hapo kesho huku mkataba huo ukihusisha jumla ya hekari 1804 zitakazotumiwa kwa kilimo pamoja na ujenzi wa viwanda viwili ndani ya eneo hilo huku pia kodi itakayolipiwa ni dola 120 kwa mwaka huu.