Boma Hai FM
Boma Hai FM
18 April 2026, 3:50 pm

Wananchi wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wameaswa kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuchangia nguvu kazi na kuilinda, ili kuhakikisha inakamilika kwa ufanisi na kuleta manufaa kwa jamii pamoja na vizazi vijavyo, Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kwa kutoa zaidi ya shilingi milioni 78 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya vyoo katika shule za msingi Mulama na Mkwamatu, huku viongozi wakisisitiza uwajibikaji, uzalendo na matumizi sahihi ya fursa za kiuchumi zinazotokana na miradi hiyo.
Na Anasta Urio
Hai- Kilimanjaro
Wananchi wilayani Hai Mkoani Kilimanjaro wametakiwa kutoa ushirikiano katika miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao ikiwa ni pamoja nakujitolea nguvu kazi ili kufanikisha miradi hiyo kwa ufanisi.
Hayo yamesemwa April 16 , 2026 na afisa elimu ya watu wazima wilaya Emaculata Mgaza wakati akikabidhi miradi ya maendeleo kwa shule ya msingi Mulama ambapo amekabidhi fedha za ujenzi wa matundu kumi na mbili ya vyoo na shule ya msingi Mkwamatu matundu kumi na mbili ya vyoo yatakayogharimu zaidi ya shilingi milion 78.

Ameeleza kuwa ushirikishwaji wa jamii utaimarisha ulinzi na utunzaji wa miradi Hiyo kwani wananchi wataulinda na kuuthamini kwa kuwa wanatambua umuhimu wake ambapo kutokufanya hivyo fedha hizo zitashindwa kufikia lengo .
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Machame Kaskazini Trael mboya ameishukuru serikali kwa kuleta fedha katika kata hiyo na kuwataka wananchi wa eneo hilo kutumia fursa hiyo kujinufaisha kiuchumi kwa kuomba nafasi mbalimbali za kazi katika mradi huo.
Nae afisa maendeleo ya jamii Tahafifu Shoo ameeleza kuwa wananchi wanapaswa kuwa mabalozi wazuri katika kulinda na kutunza miradi iliyopo kwenye maeneo yao kwani miradi inatekelezwa na serikali kwani lengo ni kunufaisha jamii iliyopo na vizazi vijavyo.
Hata hivyo Mwenyekiti wa kijiji cha mulama Evarest Kweka amesema kuwa yeye yupo tayari kujitolea anapohitajika na amewataka wananchi kushirikiana kwa pamoja ili kufanikisha mradi huo kwa wakati jamii zingine nao wapate kupata miradi hiyo.
Nao wananchi waliojitokeza kwa ajili ya kupokea mradi huo wameeleza historia ya shule hizo huku wakiishukuru serikali kwa kukumbuka shule hizo huku wakiiomba serikali ikamilishe ujenzi wa Nyumba za walimu Ili kuweka mazingira Rafiki na salama ya kazi kwa watumishi .