Boma Hai FM
Boma Hai FM
22 May 2026, 9:10 am

Wajasiriamali wa kata ya Bomang’ombe wamepatiwa mafunzo maalumu ya kulinda mitaji yao na vipato vyao pamoja na kuanzisha biashara kwa mitaji midogo, wamefundishwa kutengeneza batiki, sabuni ushonaji na mafunzo mengine ya ujasiriamali.
Na Henry keto, Hai-Kilimanjaro
Diwani wa Kata ya Bomang’ombe, Mhe. Evodi Njau, amefungua rasmi mafunzo ya ujasiriamali yanayowezeshwa na Chuo cha Mafunzo Maalumu, huku akitoa wito kwa wajasiriamali kutumia fursa hiyo kuimarisha maisha yao kwa kulinda vipato na kuanzisha mitaji mipya.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo May 21,2026 yaliyofanyika katika Ukumbi wa Klasta uliopo Shule ya Msingi kibaoni Kata ya Bomang’ombe, Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Mhe. Njau amesema wajasiriamali wanapaswa kufanya biashara kwa ujasiri bila kuogopa changamoto za ufinyu wa mitaji au kuwategemea watu wengine.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo wa Kata ya Bomang’ombe, Joyce Masawe, amewapongeza wananchi waliojitokeza kushiriki mafunzo hayo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa kata hiyo.
Masawe alisema mafunzo hayo yana mchango mkubwa kwa jamii kwani huwajengea uwezo wa kujiajiri, kuongeza kipato na kuwapatia fursa ya kupata mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na serikali bila riba

Naye Mkufunzi Mkuu wa mafunzo hayo Saravai Rashid Izina amesema kuwa mafunzo ya siku tatu yatawasaidia washiriki kutambua fursa mbalimbali za biashara na kuwawezesha kujikwamua kiuchumi.
Alisema kuwa maarifa yatakayotolewa yatawasaidia wajasiriamali kuondokana na umasikini, akisisitiza kuwa mtaji unaweza kuanzia kwenye rasilimali ndogo zilizopo mikononi mwao.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wamemshukuru Diwani wa Kata ya Bomang’ombe kwa kuona umuhimu wa kuwawezesha wajasiriamali, wakisema elimu hiyo itawasaidia kuongeza ujuzi, kuboresha mitaji yao na kufanya biashara hata kwa mtaji mdogo.
Washiriki hao walieleza matumaini yao kuwa mafunzo hayo yatakuwa mwanzo wa mabadiliko chanya katika shughuli zao za kiuchumi na kuinua vipato vya familia zao