Boma Hai FM
Boma Hai FM
29 June 2026, 7:54 am

Wananchi wamekumbushwa umuhimu wa kula mlo kamili, kudumisha usafi wa mazingira na kushiriki mapokezi ya Mwenge wa Uhuru utakaopitia wilayani Hai, huku miradi ya maendeleo ikitarajiwa kuzinduliwa.
Na Elizabeth Mafie
Hai- Kilimanjaro
Wananchi wa kijiji cha Kwasadala kata ya Masama kusini wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wameaswa kuzingatia ulaji wa makundi mbalimbali ya vyakula ili kuimarisha zaidi afya zao jambo litakalowafanya wazidi kujikita zaidi katika suala la maendeleo.
Akizungumza na wananchi hao katika maadhimisho ya lishe ambayo hufanyika kila baada ya miezi mitatu Afisa Lishe kutoka kata ya Masama Kusini Irene Shoo amesema kuwa ulaji wa makundi mbalimbali ya vyakula unaongeza uimara wa afya za wananchi pamoja na kuusaidia mwili kutokupata magonjwa mbalimbali.

“Tukizingatia lishe bora na ulaji wa makundi yale sita ya vyakula ikiwemo vyakula vyenye Protini, wanga, mbogamboga, matunda na maji itasaidia miili yetu kuwa imara na kama hatusumbuliwi na magonjwa basi tunaweza kujikita zaidi katika uzalishaji na shughuli nyingine za kimaendeleo”. Amesema Irene Shoo
Kwa upande wake Afisa mtendaji wa kijiji cha Kwasadala Edwine Lamtey amesema kuwa maadhimisho hayo hufanyika kila baada ya miezi mitatu ikiwa ni njia ya kuikumbusha jamii juu ya kuzingatia mlo bora.
“Mambo ya lishe bora ni msingi wetu bora wa maendeleo maana hakuna maendeleo bila lishe bora, na hapa tunazungumzia ulaji wa makundi yale ya vyakula, usafi wa mazingira pamoja na uwepo wa vyoo bora katika makazi yetu”. Amesema Lamtey
Katika hatua nyingine Lamtey ametumia nafasi hiyo kuwahamasisha wananchi wa kijiji cha Kwasadala kushiriki katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru ambao unatarajiwa kuwasili wilaya ya Hai Julai 3,2026
“Nawaomba wote pia tushiriki kuupokea mwenge wa uhuru wilayani kwetu na zaidi katika kijiji cha kwasadala tutakuwa na miradi miwili ambayo ni mradi wa maji pamoja na kiwanda binafsi; kwa mantiki hiyo tujitokeze kwa wingi katika maeneo ya barabarani na hata maeneo ya miradi”Amesema Lamtey