Boma Hai FM

Saashisha ahoji hatima ujenzi chuo na kituo cha afya Narumu

20 June 2026, 10:07 am

Pichani ni Mbunge wa jimbo la Hai (picha kwa msaada wa mtandao)

Serikali imewahakikishia wananchi wa Narumu na Jimbo la Hai kwa ujumla kuwa juhudi zinaendelea kuhakikisha mradi wa ujenzi wa Chuo cha Afya Narumu na Kituo cha Afya unapata fedha za kutosha ili kukamilika kwa wakati.

Na James Gasindi

Dodoma

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na Wizara ya Afya ili kuharakisha upatikanaji wa fedha za ujenzi wa Kituo cha Afya na Chuo cha Afya Narumu kilichopo katika Jimbo la Hai, mkoani Kilimanjaro.

Kauli hiyo imetolewa Juni 17,2026 bungeni na Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Sei, wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Hai, Saashisha Mafuwe, aliyetaka kufahamu ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa miradi hiyo.

Saashisha ameeleza kuwa wananchi wa Narumu walihamasika kushiriki katika utekelezaji wa mradi huo baada ya Serikali kutoa ahadi ya kujenga kituo na chuo hicho, ambapo walichangia nguvu kazi, vifaa vya ujenzi na kuanzisha msingi wa majengo yanayotarajiwa kutumika.

Sauti ya mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe.

Akijibu hoja hiyo, Dkt. Sei alisema Serikali inatambua umuhimu wa vyuo vya afya katika kuzalisha wataalamu wa afya wanaohitajika nchini na kwamba mawasiliano kati ya TAMISEMI na Wizara ya Afya yanaendelea ili kuharakisha utekelezaji wa mradi huo.

Sauti ya naibu waziri wa ofisi ya waziri mkuu, tawala za mikoa na serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Sei,

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa Chuo cha Afya Narumu kutasaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa afya na kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Pichani ni naibu waziri wa ofisi ya waziri mkuu, tawala za mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Sei (picha kwa msaada wa mtandao)