Boma Hai FM
Boma Hai FM
30 July 2026, 2:51 pm

Kamati ya Fedha, Uchumi na Mipango ya Halmashauri ya Wilaya ya Hai imehimiza ushiriki wa wazawa na wadau wa maendeleo katika kuchangia utekelezaji wa miradi ya kijamii, huku pia ikisisitiza umuhimu wa kulinda maeneo ya umma kwa kuyapima na kuyapatia hati za ardhi ili kuzuia uvamizi na migogoro.
Na Elizabeth Mafie
Hai – Kilimanjaro
Wadau wa maendeleo pamoja na wazawa wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro wametakiwa kushirikiana na Serikali kwa kujitolea kuchangia ujenzi wa shule, zahanati na miundombinu ya barabara ili kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.
Wito huo umetolewa Julai 29, 2026 na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha, Uchumi na Mipango, Edmund Rutaraka, wakati akihitimisha ziara ya siku mbili ya kamati hiyo ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Hai.

Katika siku ya mwisho ya ziara hiyo, kamati imetembelea miradi mbalimbali ikiwemo kivutio cha utalii cha Chemka pamoja na maeneo yanayomilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Hai, kwa lengo la kujionea utekelezaji wa miradi hiyo na huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akizungumzia ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Losaa, Rutaraka amesema mradi huo unatekelezwa kwa ufadhili wa mdau wa maendeleo ambaye ni mzawa wa kijiji hicho huku akiwataka wadau wengine pamoja na wazawa kuiga mfano huo kwa kujitolea kuchangia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.
Aidha amesema kamati hiyo imemwelekeza Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Hai kuhakikisha maeneo yote yanayomilikiwa na halmashauri yanapatiwa hati ili yawe salama na kuepeuka uvamizi wa wananchi.

Kwa upande wake kaimu afisa ardhi wa wilaya ya Hai Clement Mgullu amesema ni muhimu Halmashauri na Serikali kuhakikisha maeneo yote inayoyamiliki yanapata hati za ardhi ili kuzuia migogoro isiyo ya lazima kati ya Serikali na wananchi, pamoja na kulinda maeneo ya umma dhidi ya uvamizi.