Boma Hai FM

Dc Bomboko awataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya El Nino

3 September 2026, 11:52 am

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassani Omary Bomboko (kushoto) akisalimiana na mwananchi wakati alipofanya ziara katika maeneo yenye changamoto wakati wa mvua( picha na Richard Salema)

Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko amesisitiza ushirikiano kati ya viongozi na wananchi katika kufungua mitaro na njia za maji, huku akiwataka wakazi wa maeneo hatarishi kuchukua tahadhari mapema kwa kuhama kwa muda na kulinda mali zao dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na mvua za Elnino zinazotarajiwa kunyesha hapa nchini.

Na Richard Salema & Gervas Mosha

Hai – Kilimanjaro

Mkuu wa wilaya  ya Hai mkoani Kilimanjaro Hassan Bomboko, amezitaka mamlaka na wananchi kuchukua tahadhari na hatua za haraka kukabiliana na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha, ili kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza kutokana mvua   hizo za El Nino.

Bomboko ameyasema hayo Agosti 31 2026, wakati wa ziara ya kukagua maeneo yenye changamoto pindi mvua zinaponyesha  katika kata za Muungano, Bomang’ombe na Bondeni wilayani Hai.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Omary Bomboko pamoja na viongozi mbalimbali wa halmashauri ya wilaya ya Hai na wananchi.( picha na Richard Salema)

Amesema hatua hizo zinapaswa kuhusisha utoaji wa elimu kwa wananchi kuhusu tahadhari dhidi ya mvua, pamoja na ushirikiano kati ya mamlaka na wananchi katika kufungua mitaro na njia za maji ili kuzuia maji kutuama na kuingia katika makazi huku akiwataka  wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi kuhama kwa muda,pamoja na kuhamisha  mifugo na vitu vinavyoweza kuharibika ili kuepusha hasara.

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko.

Aidha amemtaka Meneja wa TARURA kushirikiana na wananchi katika kutengeneza mitaro na njia za maji, huku viongozi wa mji mdogo, kata, vijiji na vitongoji wakihakikisha njia za maji zinafunguliwa kutoka yanapotokea hadi yanapoishia.

Kwa upande wao, wananchi wameomba hatua zichukuliwe kukabiliana na changamoto zinazochangia maji kuingia katika makazi , huku mkazi wa Gezaulole, Japhet Urasa,akiishauri serikali kushughulikia makazi yaliyojengwa katika maeneo yanayozuia njia za maji.

Pichani ni mwananchi akizungumza wakati mkuu wa wilaya ya Hai alipofanya ziara katika maeneo yanakuwa na changamoto wakati wa mvua(picha na Richard Salema)

Naye Hilda Mushi amewataka wananchi kushirikiana kufanya usafi na kuboresha mazingira, hususan kufungua njia za maji, ili kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua za El Nino zinazotarajiwa kunyesha.

Sauti ya mwanachi Hilda Mushi.

Bomboko amesema serikali itaendelea kufuatilia hali hiyo na kuchukua hatua za haraka kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao unalindwa, huku akisisitiza kuwa endapo miundombinu itaathiriwa, hatua zichukuliwe kuhakikisha wanafunzi wanapata maeneo salama ya kuendelea na masomo.