Boma Hai FM
Boma Hai FM
27 August 2026, 9:17 am

Jeshi la Polisi wilaya ya Hai kitengo cha Polisi jamii limetoa elimu kuhusu kupinga uhalifu na matumizi ya madawa ya kulevya katika shule ya sekondari Lyamungo na katika jamii.
Na Henry Keto
Jeshi la Polisi Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, kupitia Kitengo cha Polisi Jamii, limetoa elimu kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lyamungo kuhusu madhara ya vitendo vya kihalifu, matumizi ya dawa za kulevya pamoja na umuhimu wa kuzingatia nidhamu ya msomo shuleni.
Elimu hiyo imetolewa Agosti 24, 2026, katika Shule ya Sekondari Lyamungo, ambapo mkuu wa Polisi Wilaya ya Hai, OCD SSP Suzan Kidiku, amewataka wanafunzi kuachana na vitendo vyote vya kihalifu na matumizi ya dawa za kulevya, akisisitiza umuhimu wa kulinda mustakabali wao.
SSP Suzan Kidiku amesema matumizi ya dawa za kulevya pamoja na utovu wa nidhamu vinaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa ufaulu wa mwanafunzi na uwezo wake wa kujifunza. Aidha, ameeleza kuwa baadhi ya vitendo hivyo vinaweza kuwa kikwazo kwa vijana kupata fursa mbalimbali za ajira na maendeleo baada ya kumaliza masomo.

Ametoa wito kwa wanafunzi hao kutumia fursa waliyonayo ya kupata elimu kwa kujituma katika masomo, kuwa na nidhamu na kuepuka makundi au vitendo vinavyoweza kuharibu maisha yao, ili waweze kujenga uwezo na kufikia ndoto zao hapo baadaye.
Nao wanafunzi wa shule ya sekondari lyamungo wameshukuru ujio wa polisi hao katika shule yao, kwani imewapa hamasa ya kusima kwa bidii ili kutimiza ndoto zao, pamoja na kuahidi kulinda amani ya nchi na pamoja na kuepuka matumizi ya madawa ya kulevya
