Boma Hai FM

Wananchi Hai watakiwa kuandaa mazingira ya kudhibiti ukatili

12 December 2023, 9:12 pm

Wadau mbalimbali wakiwa katika kilele cha kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia (Picha na Anasta Urio)

Wananchi Hai wametakiwa kuwajibika kuzuia ukatili wa kijinsia katika jamii.

Na Anasta Urio

Wananchi wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wametakiwa  kuandaa mazingira ya kudhibiti  vitendo vya ukatili katika jamii  bila kujali siasa, dini pamoja na ukabila  ili kuhakikisha kila mtu anawajibika  kupinga na kuzuia ukatili  wa kijinsia.

Hayo yamesemwa na mgeni rasmi  Nsajigwa Ndagile kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Hai Amir Mkalipa katika mkutano wa maadhimisho ya kilele cha kampeni ya siku  16 za kuzuia ukatili wa kijinsia iliyokuwa na kaulimbiu ya “Wekeza kupinga ukatili wa kijinsia” iliyofanyika  katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya Hai.

Aidha Ndagile ametoa pongezi kwa wadau mbalimbali walioshiriki katika kuhamasisha na kukamilisha  kampeni hiyo tangu ilipoanza hadi kufikia siku ya kilele na kwamba wanatakiwa kuendelea  kutoa elimu zaidi ili jamii izidi kuelimika.

Kwa upande wake mwalimu mkuu wa shule ya msingi Bomani, Nyangi Ikwabe amesema kuwa ukatili wa kijinsia unaweza kufanywa na mtu yeyote  na kuleta madhara katika jamii na kuwataka wazazi kutimiza wajibu wao kwa watoto ili kuwalinda dhidi  ya  ukatili wa kijinsia.

Naye mwenyekiti wa jukwaaa la mwanamke wilaya ya Hai Etropia Assenga amesema kuwa kuna aina nyingi za ukatili ikiwemo ukatili wa kingono, ukatili wa kiuchumi, ukatili wa kimwili na ukatili wa kisaikolojia ambao umekuwa ukiwaathiri zaidi wanaume.

Sauti ya mwenyekiti wa jukwaa la wanawake wilaya ya Hai Etropia Assenga alielezea aina za ukatili na namna ambavyo wanaume wanaathirika na ukatili huo.