Boma Hai FM

Dc Bomboko azindua kampeni chanjo ya polio,watoto zaidi ya elfu 63 kufikiwa

28 August 2026, 7:55 am

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko akimpatia mwanafunzi wa shule ya msingi Bomani chanjo ya polio ya matone katika uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika hospitali ya wilaya ya Hai( picha na Elizabeth Mafie)

Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko amesisitiza umuhimu wa chanjo ya polio ya matone kwa watoto chini ya miaka 10, huku Mganga Mkuu wa Wilaya akieleza kuwa zaidi ya watoto 63,000 wanalengwa kufikiwa katika kampeni hiyo ,Viongozi wazazi na walimu wahamasishwa pamoja ushiriki wa jamii katika kufanikisha zoezi hilo.

Na Anasta Urio

Hai – Kilimanjaro

Wananchi wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wametakiwa kuwapa ushirikiano wataalamu wa afya katika utekelezaji wa kampeni ya chanjo ya matone ya polio, kwa kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo hiyo kwa wakati.

Wito huo umetolewa na mkuu  wa wilaya  ya Hai Hassan Bomboko, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya chanjo ya polio iliyofanyika Agosti 27, 2026 katika Hospitali ya Wilaya ya Hai, ambapo amewataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapatiwa chanjo hiyo ili kuwalinda dhidi ya ugonjwa wa polio.

Pichani ni mganga mkuu wilaya ya Hai Dkt Itikija Msuya akimpatia chanjo ya polio ya matone mtoto ,katika uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika hospitali ya wilaya ya Hai(picha na Elizabeth Mafie)

Bomboko amesema kinga ni bora kuliko tiba, hivyo Serikali imeamua kuwakinga watoto wenye umri chini ya miaka 10 kama sehemu ya jitihada za kulinda afya ya kizazi cha sasa na kijacho, akisisitiza kuwa chanjo hiyo ni salama kwa afya.

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko.

Kwa upande wake mganga mkuu wa Wilaya ya Hai Itikija Msuya, amesema kampeni hiyo inalenga kuwafikia zaidi ya watoto elfu 63 wenye umri chini ya miaka 10 ili wapatiwe chanjo ya polio, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuzuia maambukizi na kuhakikisha taifa linakuwa salama dhidi ya ugonjwa huo.

Sauti ya mganga mkuu wilaya ya Hai Dkt Itikija Msuya.

Naye mwenyekiti  Halmashauri ya wilaya  ya Hai Edimundi Rutaraka, amewahimiza wananchi kujitokeza katika vituo vilivyopangwa kwa ajili ya chanjo hiyo, akisema chanjo ipo ya kutosha huku akiwataka wanaume kujitokeza kuwasindikiza wanawake katika vituo vya kutolea chanjo ili kutoa ushirikiano katika malezi ya familia na kufanikisha zoezi.

Sauti ya mwenyekiti halmashauri ya wilaya ya Hai Edmund Rutaraka.
Pichani ni mwenyekiti halmashauri ya wilaya ya Hai Edmund Rutaraka akimpatia chanjo ya polio ya matone mtoto,katika uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika hospitali ya wilaya Hai(picha na Elizabeth Mafie)

Vilevile mwalimu Nyange Ikwabe wa Shule ya Msingi Bomani, aliyewaleta wanafunzi wake kupatiwa chanjo ya polio, amewataka wazazi kuwa na moyo wa kuipokea chanjo hiyo, akisema lengo la Serikali ni kulinda afya za watoto.

Sauti ya Nyange Ikwabe mwalimu wa shule ya msingi Bomani.
Pichani ni wazazi mbalimbali waliojitokeza kuwaleta watoto wao kwa ajili ya kupata chanjo ya polio ya matone katika uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika hospitali ya wilaya ya Hai(picha na Elizabeth Mafie)

Kwa upande wao, wazazi waliojitokeza katika zoezi hilo, akiwemo Nickolaus Marwa, amewahimiza wazazi wote kuhakikisha wanawapeleka watoto wao kupata chanjo ya polio kwa ajili ya kuwalinda dhidi ya ugonjwa huo.

Sauti ya Nickolaus Marwa , mzazi aliyeleta mtoto kwa ajili ya kupata chanjo ya polio ya matone.

Baadhi ya watoto waliojitokeza kupatiwa chanjo hiyo, wakiwemo wanafunzi wa Shule ya Msingi Bomani, Getruda Fadhili na Ikram Said, wamesema wamefika hospitalini ili kupata chanjo itakayowakinga dhidi ya ugonjwa wa polio.

Sauti ya watoto waliojitokeza kupata chanjo ya polio ya matone.
Pichani ni wanafunzi mbalimbali waliofika kwa ajili ya kupata chanjo ya polio ya matone(picha na Elizabeth Mafie)