Boma Hai FM
Boma Hai FM
15 April 2026, 2:44 pm

Ziara ya Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi (TISEZA) wilayani Hai imelenga kuhamasisha vyama vya ushirika kuwekeza kwa tija, kutafuta vyanzo mbadala vya kipato na kupata masoko ili kukabiliana na changamoto za tabia nchi na kuboresha maisha ya wakulima
Na Anasta Urio
Hai- Kilimanjaro
Vyama vya ushirika (AMCOS) wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro vimetakiwa kufanya uwekezaji wenye tija kwenye mashamba ya ushirika ili kunufaisha vyama na taifa kwa ujumla.
Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka ya uwekezaji na maeneo maalumu ya kiuchumi (TISEZA) Giliad Teri ameyasema hayo wakati wa ziara ya kutembelea, kutoa elimu na ushauri kwa vyama vya ushirika kufuatia ombi lililotolewa na Mbunge wa Jimbo la Hai Saashisha Mafuwe.
Teri ameeleza kuwa ili vyama vya ushirika viendelee kuwa na uwekezaji wenye matokeo chanya kwa pande zote kwa mwekezaji na vyama vya ushirika ni lazima viwe na mbinu mbadala wa mapato ili kutatua changamoto za masoko na mabadiliko ya tabia nchi.
Nae Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Kilimanjaro Jackline Senziga ameviasa vyama hivyo kutumia TISEZA kwa ufasaha katika kutafuta masoko ya mazao na bidhaa mbali mbali zinazotokana na ushirika.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmshauri ya wilaya ya Hai Edmund Rutaraka ambaye katika ziara hiyo alimwakilisha Mbunge wa jimbo la Hai amesema ziara hiyo itasaidia vyama hivyo na wawekezaji kupata elimu na uelewa wa fursa mbalimbali ambazo zipo kwenye mashamba ya ushirika pamoja na changamoto ambazo zinaweza kutatuliwa na bodi husika kama kuwekeza kwenye mazao tofauti na kahawa ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kama ukame.
Nae Meneja wa kampuni ya uwekezaji ya APKL Donald Temba amemshukuru Mbunge kwa ziara hiyo na kuomba TISEZA iwasaidie kupata soko la uhakika (direct export) ili wakulima wa zao la kahawa wanufaike na kupata hamasa zaidi ya kulima zao hilo.