Boma Hai FM
Boma Hai FM
25 July 2026, 8:31 am

Mbali na kueleza mafanikio ya miradi ya maendeleo, Mbunge Saashisha amesisitiza umuhimu wa kulinda maeneo ya kimkakati na kuhakikisha changamoto za maji zinapatiwa ufumbuzi.
Na Oliver Joel
Hai – Kilimanjaro
Mbunge wa Jimbo la Hai mkoani Kilimanjaro Saashisha Mafuwe, amewataka wananchi wilayani Hai kutumia kikamilifu fursa zinazotokana na miradi ya maendeleo inayotekelezwa na serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuboresha maisha yao.

Akizungumza Julai 24, 2026 katika kipindi maalum kupitia Redio Boma Hai FM, Saahisha amesema miongoni mwa miradi hiyo ni mradi wa ufugaji wa kisasa unaofadhiliwa na washirika kutoka Uholanzi, unaolenga kuwahamasisha wafugaji kutumia mbinu za kisasa ili kuongeza tija na kipato.
Aidha amesema miradi mbalimbali ya maendeleo inaendelea kutekelezwa wilayani Hai, huku akiwasihi wananchi wanaoishi pembezoni mwa barabara ya Bomang’ombe–TPC kutouza maeneo yao kwa kuwa ni eneo la kimkakati linalotarajiwa kunufaika na uwekezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Kuhusu huduma ya maji Saashisha amesema serikali imeendelea kuwekeza katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya maji, ikiwemo mradi wa shilingi bilioni 3.39 ambao umekamilika pamoja na mradi wa shilingi milioni 900 uliotekelezwa eneo la Kwasadala kwa lengo la kupunguza adha ya upatikanaji wa maji kwa wananchi.
Akijibu swali la msikilizaji aliyepiga simu kuhusu ukosefu wa maji katika Shule ya Msingi Kingereka, Saashisha amemuagiza Meneja wa Ruwasa Wilaya ya Hai kushughulikia changamoto hiyo ili wanafunzi pamoja na wananchi wanaozunguka shule hiyo waweze kupata huduma ya maji safi na salama.