Boma Hai FM
Boma Hai FM
18 April 2026, 2:52 pm

Katika kuendelea kutunza na kuhifadhi mazingira,shirika la KCEO limefanya zoezi la upandaji miti katika shule sita za wilaya ya Hai.
Na Elizabeth Mafie
Hai Kilimanjaro
Wanafunzi katika shule sita za wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro wametakiwa kutunza miti iliyopandwa katika shule zao ili kufikia lengo la utunzaji wa mazingira.

Wito huo umetolewa Aprili 17, 2026 katika Shule ya Sekondari Hai Day na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Trael Mboya alipomwakilisha Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Edmund Rutaraka katika zoezi la upandaji miti lililofanyika katika shule mbalimbali za wilaya ya Hai ikiwemo Shule ya Hai Day, Bomang’ombe,Mukwasa, Nronga , shule ya wasichana Masama pamoja na shule ya msingi Mtakuja.
Zoezi hilo limefanywa kwa ushirikiano na Shirika lisilo la kiserikali la Kilimanjaro Community Empowerment Organization (KCEO) lenye makao yake wilayani Hai ambalo limefanikiwa kuotesha miti elfu moja katika shule hizo sita kwa lengo la kuhamasisha utunzaji na ulinzi wa mazingira.

Akizungumza katika zoezi hilo Mboya amesema kuwa ili kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kulinda na kuhifadhi mazingira, ni muhimu kwa wanafunzi kuhakikisha miti hiyo inatunzwa na kukua ili iweze kuleta manufaa ikiwemo kuboresha hali ya hewa na kuongeza uoto wa asili huku akilishukuru shirIka la KCEO kwa kuamua kutunza mazingira kwa kupanda miti katika shule mbalimbali za wilaya ya Hai .
Kwa upande wake Katibu wa shirika hilo Odette Ngulu amesema lengo la KCEO ni kutunza mazingira kwa njia mbalimbali mojawapo ikiwa ni kupanda miti pamoja na kueneza teknolojia rahisi zinazosaidia kupunguza uharibifu wa mazingira kama kukata miti kwa ajili ya biashara ya mkaa,ili jamii iweze kutumia nishati mbadala ,kuwa na teknolojia inayowasaidia jamii kufanya biashara na kutengeneza kipato na kupata uhakika wa chakula na lishe kwa njia rahisi bila kuharibu mazingira.
Ngulu ameongeza kuwa jamii ya sasa imekuwa ikikata miti kwa ajili ya kupata mkaa na kuni kwa ajili ya kufanya biashara ili kuweza kuendesha maisha lakini zipo njia mbali mbali za kuweza kujitengenezea kipato ili kuweza kuhifadhi mazingira.

Naye afisa maliasili wilaya ya Hai Mbayani Mollel amesema kuwa wilaya ya Hai miti inapandwa ya kutosha na miti hiyo inastawi na kwamba ofisi ya maliasili wilaya ya Hai imeendelea kutoa elimu katika makundi mbalimbali ili kufanikisha utunzaji wa miti hiyo na mpaka sasa lengo la kupanda miti milioni moja na nusu limetimia kutokana na ushirikiano kuanzia ngazi ya kitongoji ya eneo husika.
Mollel ameongeza kuwa ushiriki wa wanafunzi katika shughuli za mazingira ni hatua muhimu ya kujenga jamii inayojali na kuthamini rasilimali za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Miongoni mwa shule zilipanda miti ikiwemo shule ya sekondari Mukwasa na shule ya Sekondari Hai Day wakuu wa shule hizo walipata fursa ya kushukuru shirika la KCEO kwa kuchagua shule hizo na kupanda miti kwani wanafunzi watajisomea katika mazingira tulivu na salama.

Wanafunzi katika shule hizo wamehaidi kutunza miti hiyo na kuifatilia kwa ukaribu ili iweze kuwanufaisha wao na hata wananfunzi wengine watakaokuja kusoma katika shule hizo.