Boma Hai FM
Boma Hai FM
26 August 2026, 3:57 pm

Mkuu wa Wilaya ya Hai, Hassan Bomboko, amesisitiza ushirikiano wa viongozi wa serikali, dini na jamii katika kuhamasisha wazazi na walezi kuwapeleka watoto walio chini ya miaka 10 kupata chanjo ya polio, huku zoezi hilo likitarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 27 hadi 30, 2026.
Na Gervas Mosha
Hai – Kilimanjaro
Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko amewataka viongozi na watendaji katika ngazi za kata na vijiji kuongeza kasi ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kampeni ya chanjo ya polio, inayotarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 27 hadi 30, mwaka huu.
Bomboko amesema viongozi wanapaswa kutumia siku zilizobaki kabla ya kuanza kwa kampeni hiyo kuhakikisha taarifa sahihi zinawafikia wazazi na walezi wenye watoto walio chini ya umri wa miaka 10, ili watoto hao wajitokeze na kupata chanjo.
Amesema chanjo hiyo ni haki ya kila mtoto mwenye umri chini ya miaka 10, hivyo ametoa wito kwa serikali, viongozi wa jamii, viongozi wa dini, wazazi, walezi, vyama vya siasa na taasisi binafsi kushirikiana katika kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kuhusu umuhimu wa chanjo hiyo.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Wilaya ya Hai Dkt Itikija Msuya amesema Halmashauri imejipanga kuhakikisha hakuna mtoto aliye chini ya umri wa miaka 10 anayekosa chanjo katika kampeni hiyo.
Nae afisa afya wa wilaya ya Hai George Masawe, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha watoto wote walio katika kundi lengwa wanapata chanjo.
Kampeni hiyo itafanyika kuanzia Agosti 27 hadi 30 mwaka huu, huku wananchi wakihimizwa kutoa ushirikiano kwa timu za afya zitakazohusika katika utekelezaji wa zoezi hilo.
