

19 March 2025, 8:57 pm
Ili kukabiliana na changamoto ya uchumi kwenye jamii taasisi binafsi nchini zinatakiwa kutambua nafasi ya mwanamke.
RUNGWE-MBEYA
Na Lennox Mwamakula
Shirika la SHE CAN Foundation chini ya mkurugenzi wake, ambaye pia ni Mbunge wa viti Maalumu Mkoa wa Mbeya, Sophia Mwakagenda limekabidhi cherehani 15 kwa wanawake na wasichana 15 waliohitimu mafunzo ya ushonaji ndani ya kituo hicho.
Imeelezwa kuwa shirika hilo limekuwa likipokea wanawake na wasichana kwaajili ya kujifunza ushonaji kozi inayotolewa kwa muda wa miezi mitatu kituoni hapo.
Akizungumza mara baada ya kukabidhi cherehani hizo diwani wa kata ya Kinyala Joseph Mwapongo ameahidi kumuunga mkono Mbunge Mwakagenda ili kuhakikisha cherehani hizo zinaendelea kutolewa na kwa wanafunzi wengine wanaoendelea kujifunza kituoni hapo.
Awali akisoma risala mbele ya mgeni rasmi mratibu wa kituo hicho Abraham Nzunda amesema kituo hicho kimeanzishwa miaka mitano iliyopita na mpaka sasa kimetoa mafunzo kwa wanawake na wasichana 336 huku lengo kuu ikiwa ni kuhakikisha wanufaika wanajikwamua kiuchumi kupitia elimu waliyopata.
Kwa upade wake Mchungaji Ans Sankey ambaye ni mwenyekiti wa bodi kituoni hapo amewapongeza wanafunzi hao waliomaliza mafunzo na kupewa vitendea kazi vitakavyowasaidia kujikwamua kichumi.
Naye Mkurugenzi wa Shirika la She can Foundation, ambaye ni Mbunge wa viti Maalumu Mkoa wa Mbeya, Sophia Mwakagenda amesema cherehani hizo ni ufadhili kutoka kwa mfadhili anayeishi nchini Japan ambaye alipata nafasi ya kufika kituoni hapo na kutoa mafunzo, huku akiwataka kwenda kuvitumia kwa malengo yaliyokusudiwa.