GHATI MEGEWA
Orkonerei FM

Simanjiro Kuwafikia Watoto Zaidi ya Laki 1 Chanjo ya Polio

24 August 2026, 11:15 am

GHATI MEGEWA
Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma (DHO) Wilaya ya Simanjiro, Ghati Megewa, akifafanua maandalizi na ratiba ya kampeni kabambe ya chanjo ya polio inayotarajiwa kuanza hivi karibuni mkoani Manyara. Ghati anawasihi wazazi kutoa ushirikiano. (Picha na Isack Dickson)

Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro inatarajia kuwafikia watoto 116,152 chini ya umri wa miaka 10 kwenye Kampeni Maalum ya Chanjo ya Polio itakayofanyika kwa awamu mbili kuanzia mwezi huu wa Agosti.

Na Dorcas Charles

Mkoa wa Manyara, kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, uko katika maandalizi kabambe ya kuendesha Kampeni Maalum ya Chanjo ya Polio inayolenga kuwalinda watoto dhidi ya ugonjwa huo unaosababisha kupooza.

Katika mahojiano maalum, Ghati Megewa, Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma na Afya ya Jamii kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, anaeleza kuwa kampeni hiyo itafanyika kwa awamu mbili na inatarajia kuwafikia jumla ya watoto 116,152 wilayani humo.

Ratiba ya Kampeni:

  • Awamu ya Kwanza: Tarehe 27 hadi 30 Agosti (Siku 4)
  • Awamu ya Pili: Tarehe 29 Septemba hadi 01 Oktoba (Siku 4)
Laigwanani Godson Nduya Lukumay kutoka Terrat, Simanjiro, akiwa studioni kutoa wito kwa jamii na viongozi wenzake wa kimila kuunga mkono kampeni ya chanjo ya polio. Msisitizo wake ni kulinda afya ya mtoto kama msingi wa kesho ya jamii. (Picha na Isack Dickson).

Naye Mzee wa Kimila kutoka Terrat, Simanjiro, Bwana Godson Nduya Lukumay, ametoa wito kwa jamii, wazazi na walezi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wahudumu wa afya watakaopita nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha kila mtoto anayestahili anapata chanjo hiyo salama.