Orkonerei FM

Malaigwanani wabadilisha mtazamo hasi juu ya wanawake jamii ya kimaasai

11 February 2024, 9:45 am

Alaigwanan LESIRA SAMBURI akihojiwa na mwanahabari wetu ISACK DICKSON (aliyeshika kifaa cha kurekodia) katika kijiji cha terrat wilaya ya simanjiro. (picha na Dorcas Charles)

Na Isack Dickson.

Wazee wa kimila wa jamii ya kimaasai malaigwanani (laigwanak) wamefanikiwa kubadilisha mitazamo hasi waliyokuwanayo wanajamii hao juu ya uwezo wa wanawake katika kufanya maamuzi ndani ya familia na hata kwenye jamii.

Hayo yameelezwa na mwenyekiti wa malaigwanani wilaya ya simanjiro Alaigwanani LESIRA SAMBURI wakati akizungumza na ORKONEREI FM RADIO kupitia kipindi cha NIJUZE kinachoruka kila alhamis saa 12:00 jioni.

Mzee Lesira amesema kuwa awali katika jamii ya kimasai hakukuwa na nafasi ya mwanamke kushirikishwa katika jambo lolote la kifamilia na la jamii haswa katika kufanya maamuzi.

Alaigwanan Lesira amesema kuwa kwa sasa mambo yamebadilika kwa sehemu kubwa japo bado kunachangamoto za baadhi ya familia kuendelea kushikilia mila kandamizi kwa wanawake jambo ambalo wao wanaona si zuri.