Chai FM
Chai FM
28 May 2025, 9:06 pm

Wajumbe wanaopokea rushwa kwa wagombea wamekuwa chanzo cha viongozi wasiowajibika kwa wananchi.
Na Cleef Mlelwa
Uwepo wa mifumo ya kisiasa ambayo inaamini katika kugawa vitu kwa wananchi badala ya kuwajengea uwezo utakao wasaidia kujiletea maendeleo na kujitegemea imetajwa kuwa ndio chazo cha kupatikana viongozi ambao hawatokani na wananchi.
Hayo yamesemwa na mchambuzi wa masuala ya kisiasa na uchumi mkoa wa Njombe Oraph Mhema wakati akizungumza na kituo hiki kuelekea uchaguzi mkuu ambao utafanyika oktaba mwaka huu,ambapo amesema kitendo cha wanasiasa kuamini katika kugawa vitu kwa wananchi imepelekea wale wenye sifa ya kuwa viongozi kukosa nafasi hizo kutokana na kutokuwa na fedha.
Mhema amesema katika nyakati za sasa mwenye fedha ndiye anayeamua awe diwani ama awe mbunge na kueleza kuwa mfumo huo umesababisha hata wajumbe ambao wanapiga kura za maoni kuwachagua wagombea udiwani na ubunge kutokana na uwezo wao wa kifedha badala ya kuwaongoza wananchi.
Mchambuzi huyo amesema kutokana na majukumu makubwa ya Mbunge na Diwani katika kuisimamia serikali, kutunga sheria na kupitisha mikataba mbalimbali yenye maslahi kwa taifa sifa ya kujua kusoma na kuandika pekee haitoshi.
Naye katibu wa chama cha Act-Wazalendo mkoa wa Njombe Stanely Mbembati amesema kitendo cha wagombea kutumia mbinu ya kugawa vitu na kutumia fedha ili wachaguliwe imepelekea kupatikana kwa viongozi wasio na uwezo wa kuletea wananchi maendeleo.
Nao baadhi ya wajumbe wa chama cha mapinudizi mjini Makambako,Pascal Shauri na Justini Mwangaya wamekiri uwepo wa baadhi yao wanaochagua wagombea kupitia fedha zao hali inayosababisha kupatikana kwa viongozi ambao wanajali maslahi yao binafsi kuliko ya wananchi.