Kitulo FM
Kitulo FM
5 June 2026, 6:15 pm

Kutokana na baadhi ya watu wazima kutokujua kusoma na kuandika halmashauri ya wilaya ya Makete, Idara ya Elimu ya Watu Wazima wameweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wakazi wote wa Makete wanajua kusoma na kuandika.
Na Mwandishi Wetu
Imeelezwa kuwa asilimia 14 ya watu wazima wa Wilaya Makete Mkoani Njombe hawajui kusoma kuandika na kuhesabu
Hayo yamesemwa na Afisa elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi ndg Babtisa Kaguo alipokuwa akizungumza na kitulo fm kuwa kutokana na kiwango hicho cha watu kutokujua kusoma kuandika na kuhesabu imewalazimu kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi na kuelewa program zinazoendeshwa na elimu ya watu wazima katika halmashauri ya makete ili waweze kujitokeza na kujifunza.
Aidha ndg Kuguo amesema kuwa kwamujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kuna wazazi hawajui kusoma kuandika na kuhesabu jambo linalowalizimu kuendelea kuhamasisha kujitokeza kwa wingi katika vituo vilivyopo ili waweze kujifunza kwa manufaa yao kwa ujumla.
Kaguo amesema mikakati waliyoiweka katika halmashauri ya wilaya ya Makete ni kuhakikisha asilimia 14 ya watu wazima wanajua kusoma huku akiongeza kuwa sera ya taifa ya elimu inasema kila shule ya msingi, sekondari ni kituo cha elimu ya watu wazima.

Kutokana na baadhi ya watu kuogopa kujiunga na mafunzo hayo kuhofia kunyanyapaliwa na familia au jamii, Kaguo ameeleza njia wanazotumia kuweza kuwapata watu hao na kupatiwa mafunzo yatakayowasaidia kujua kusoma na kuandika.
Afisa elimu ameeleza kuwa tayari wataalam wapatao sabini wapo ili kuhakikisha wanatoa elimu au mafunzo ya elimu ya watu wazima huku akiongeza kwa kusema kuwa baada ya kujua kusoma na kuandika kuna kisomo cha manufaa kama kupata ujuzi wa kilimo cha viazi na mengine ili kuendelea kupata ujuzi zaidi.
Afisa elimu amesema mpango uliopo ni kuweza kuhakikisha ifikapo mwezi wa tisa mwaka huu halmashauri ya wilaya ya Makete mkoani Njombe kuwe na vituo zaidi ya 30 ambapo kwa sasa vipo vituo 4 vinavyotoa mafunzo hayo ya elimu kwa watu wazima.