Mkuu wa Polisi Wilaya ya Makete A.P Mwampamba
Kitulo FM

Toeni Taarifa za Matukio ya Ukatili kwa Watoto-Jeshi la Polisi Makete

March 9, 2023, 11:03 am

Jeshi la Polisi Wilayani Makete limewataka Wazazi na walezi wa watoto kuwa karibu na watoto wao ili kuwalinda dhidi ya unyanyasaji na ukatili wa Kijinsia.

Mkuu wa Polisi Wilaya ya Makete A.P Mwampamba amesema hayo akizungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika tarehe 8 Machi, 2023 yaliyofanyika Kijiji cha Isapulano yakihudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Makete Mhe. Juma Sweda, Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Makete William Makufwe na Wananchi wa Kata ya Isapulano.

OCD Mwampamba amesema kumekuwa na matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto lakini Jamii hairipoti matukio hayo kwenye vyombo vya Sheria na kuyakalia kimya matukio yanayopelekea kufichwa kwa haki kwa watoto.

“Jamii inayaona Matukio ya watoto kupewa ujauzito lakini inamamaliza kifamilia, na watu hawaripoti matukio hayo kwenye Dawati la Jinsia wala Polisi wala Serikali ya Mtaa…hivyo tunawanyima Haki watoto wetu wanakosa hata Haki yao ya kupata Elimu

Niwaombe Wananchi hakikisheni mnaripoti kwenye mamalaka husika ili wahalifu waweze kuchukuliwa hatua za Kisheria na kufikishwa Mahakamani kujibu mashtaka”.