Kitulo FM

Madereva wa Daladala Njombe wagoma

February 6, 2023, 3:07 pm

Madereva wa daladala #Njombe mjini, wamesitisha huduma ya usafirishaji kwa kipindi kisichojulikana baada ya madereva wa bajaji kuruhusiwa kusafirisha abiria katika maeneo yote ndani ya Halmashauri ya mji wa Njombe.

Katibu Tawala wilaya ya Njombe Emmanuel George akizungumza na Madereva Daladala Njombe

Wamesema kuwa madereva wa bajaji wameshindwa kufuata Utaratibu na kuingilia Maeneo yao ya kusafirisha abiria katika mji wa Njombe huku wakisisitiza kutorejea barabarani mpaka pale Mamlaka zitakapozuia bajaji kuingilia maeneo yao ya usafirishaji ikiwemo Kibena, Nundu na Hagafilo.

Kitulo FM imezungumza na Msimamizi wa Daladala Mjini Njombe Seleman Malekela pamoja na Mwenyekiti wa Daladala Samweli Mvile ambapo wote kwa pamoja wameonekana kutoridhishwa na hatua hiyo iliyochukuliwa na Madereva wa bajaji mjini hapa.

Katibu Tawala wilaya ya Njombe Emmanuel George amefika na kuzungumza na madereva hawa huku akiwaomba kuendelea kutoa huduma wakati Serikali ikiendelea kujadili namna ya kuitafutia ufumbuzi changamoto hiyo.