Pangani FM
Pangani FM
29 August 2025, 11:31 am

“Tunaona mambo makubwa yanakwenda kutokea kwa sababu lengo kubwa la huu Uraghbishi ni kuchochea uwajibikaji.”
Na Cosmas Clement
Utekelezwaji wa program ya uraghbishi inayoendeshwa na shirika la usaidizi wa kisheria (PACOPA) kwa kushirikiana na shirika la Twaweza wilayani Pangani umetajwa kuchangia mabadiliko chanya ya kimaendeleo wilayani humu.
Hayo yamezungumzwa na Mkuu wa idara ya maendeleo ya jamii wa halmashauri ya wilaya ya Pangani Bi Sekela Mwalukasa ambapo amelipongeza shirika la Twaweza kwa kuendesha program hiyo akisema imekuwa msaada mkubwa kwa halmashauri katika kuibua changamoto na kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati mafunzo ya waraghbishi yaliyofanyika mjini Pangani, Bi Happiness Nkwera kutoka Shirika la Twaweza amesema program hiyo imeleta mafanikio katika jamii za vijiji vinavyotekeleza program hiyo.
Mratibu wa uraghbishi kutoka shirika la wasaidizi wa kisheria Pangani ‘PACOPA’ Mtumwa Kombora ameiomba Serikali kupitia viongozi wa vijiji kushirikiana kwa karibu na Wananchi ili kukuza ushirikishwaji wa wananchi katika shughuli za maendeleo.
Bibie Mohamed mwakilishi wa waraghbishi kutoka kijiji cha Msaraza wilayani Pangani, amesema kutokana na mafunzo ya uraghbishi yamewawezesha kuimarisha kufanyika kwa mikutano katika kijiji chao.

Program ya uraghabishi inatekelezwa na Shirika la usaidizi wa kisheria Pangani PACOPA kwa kushirikiana na Twaweza kwa lengo la kuwawezesha wananchi kuibua kupanga na kutekeleza vipaumbele vyao wenyewe katika vijiji.