Sibuka FM

Kituo cha kupozea umeme suluhisho sahihi kwa wakazi wa Simiyu

24 February 2026, 11:38 am

Pichani ni mkuu wa mkoa wa Simiyu,Anamringi Macha akizungumza jambo kwenye moja wapo wa shughuli za kiserikali Picha kutoka maktaba ya Sibuka fm

Tunahitaji kuwa na umeme wa uhakika ili kuvutia wawekezaji wakubwa kwenye viwanda maana hatuwezi kuwa na wawekezaji wakubwa wakati huo hatuna umeme wetu wa uhakika lazima sasa juhudi zifanyike kwa namna yoyote ile”.

Na,Daniel Manyanga 

Wakazi wa mkoa wa Simiyu wameiomba serikali kupitia shirika la umeme Tanzania TANESCO  kukamilisha ujenzi wa kituo cha kupozea umeme ili waweze kupata huduma hiyo kwa uhakika tofauti na sasa ambapo kumekuwepo na changamoto ya kukatikakatika hali inayopelekea baadhi ya vitu vyao vya ndani kuungua.

Wakizungumza na Sibuka Fm,Ali Sharifu,Amos Omolo na Wiliam Kiwango wamesema wanategemea umeme kufanya shughuli mbalimbali za kujiingizia kipato lakini wapo ambao ni wateja wa bidhaa zinazotegemea umeme hivyo kukatika kwa  umeme mara kwa mara kumekuwa changamoto kubwa kwao kufanya shughuli hizo.

Sauti ya wakazi wa Simiyu

Anamringi Macha ni mkuu wa mkoa wa Simiyu amesema kuwa wawekezaji  hususan wa viwanda wanataka umeme wa uhakika ili wafaye uwekezaji utakaowapatia tija hatua itakayowezesha kuchangia kwenye pato la Taifa kutokana na uzalishaji huo.

Sauti ya mkuu wa mkoa wa Simiyu, Anamringi Macha
Kwenye picha ni mkurugenzi mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange akizungumza na waandishi habari hawapo pichani baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha kupozea umeme Picha kutoka maktaba ya Sibuka fm

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa TANESCO,Lazaro Twange amesema mkataba wa awali ulisainiwa 2023 kutoka na changamoto mkataba wake ulivunjwa na sasa utekelezwaji wake unafanywa  na wataalamu wa ndani kutoka shirika la umeme Tanzani (TANESCO) kwa gharama ya shilingi bilioni 7 na walianza utekelezaji Oktoba 30,2025 na unatarajia kukamilika Mei 23,2026 na kwasasa umefikia asilimia 20.75.

Sauti ya Lazaro Twange mkurugenzi mtendaji wa TANESCO

Mkurugenzi  mtendaji wa shirika la umeme Tanzania Lazaro Twange akiwa Malampaka  wilayani Maswa kwenye eneo la ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme  yenye urefu wa kilomita 110 inayotoka Ibadakuli mkoani Shinyanga hadi Imalilo wilayani Bariadi mkoani hapa kilipo kituo cha kupozea umeme ,na ujenzi huo ulianza March 2023 na unatarajiwa kukamilika  Juni 30 2026 na utekelezaji wake umefikia asilimia 54.9.

Sauti ya mkurugenzi mtendaji wa TANESCO