Sibuka FM
Sibuka FM
17 February 2026, 3:45 pm

“Tunahitaji kuona miradi inayotekelezwa iwaguse moja kwa moja wananchi katika kuleta maendeleo kwenye maeneo yao ili kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja kutokana na shughuli anayoifanya”.
Na,Daniel Manyanga
Baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya ya Maswa mkoa wa Simiyu limepitisha rasimu ya mpango wa bajeti ya bilion 51 katika mwaka wa fedha 2026/2027 huku wakiahidi kusimamia kikamilifu ukusanyaji wa mapato pamoja na kubuni vyanzo vipya ya mapato ya ndani ili kuweza kutekeleza kikamilifu miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.

Akizungumza katika baraza hilo la bajeti lililoketi tarehe.16.02.2026 mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo,Maisha Mtipa amesema vipaumbele vya bajeti hiyo ni elimu,afya,kilimo na viwanda huku mwenyekiti wa halmashauri hiyo ambaye pia ni diwani wa kata ya Isanga,Miza Jishuli akiahidi kuzishughulikia changamoto mbalimbali zilizotajwa na mkuu wa wilaya ili kuleta maendeleo kwa wananchi.
Julius Ikongora ni afisa mipango wa halmashauri hiyo ametaja mkakati wa ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa mpango wa bajeti hiyo ni kuundwa kwa kikosi kazi kwa ajili ya ukusanyaji wa mapato katika maeneo ya minada,magulio na vituo vya kuuzia mazao na kusimamia utaratibu wa stakabadhi ghalani kuhamamisha kilimo cha mazao ya kimkakati ya biashara ya pamba,choroko,alizeti na mpunga na kuendelea na ujenzi wa vibanda 12 vya biashara katika eneo la stendi ya zamamni kwa lengo la kuongeza mapato ya ndani.

Kwa upande wao, baadhi ya madiwani walichangia mjadala huo wakitaka kuwepo kwa usimamizi madhubuti wa miradi ili kuondoa malalamiko ya ucheleweshaji na ubadhilifu wa fedha za umma ili kuharakisha kukamilika kwa miradi hiyo kwa manufaa ya wananchi ambao wanaimani kubwa na serikali yao.