Sibuka FM
Sibuka FM
21 January 2026, 5:58 am

“Elimu ni urithi pekee kwa mwanadamu ambao huwezi kupokomywa na mtu yeyote lakini pia kwa dunia ya sasa usipokuwa na elimu walau kidogo ni ngumu sana kufanikiwa maana siku hizi kila kitu kinahitaji elimu hivyo tuwapeleke watoto wakapate elimu maana ndiyo ufunguo wa dunia ya leo”.
Na,Daniel Manyanga
Mkuu wa wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, Simon Simalenga ameagiza wazazi na walezi wa watoto wote ambao bado hawajaripoti shuleni hadi sasa wasakwe na wachukuliwe hatua kali kwa mujibu wa sheria za nchi.
Simalenga ametoa maelekezo hayo wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara uilofanyika kata ya Gilya na kusema kuwa serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu, hivyo ni muhimu watoto wapelekwe shuleni kusoma ili waweze kutimiza ndoto zao.
Amesema kuwa haiwekani serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania inayoongozwa na rais Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan itumie pesa nyingi hivyo kuwekeza kwenye miundombinu bora ya elimu ili watoto wote wapate elimu bure halafu leo anatokea mzazi au mlezi hataki mtoto wake asome licha ya ufaulu na umri wa kuanza masomo umefika lazima sheria ifuatwe kwa watu wa namna hiyo.
Kalunde Masunga, Mabula Kulyama na Charles Gambumu, ni baadhi ya wakazi wa kata ya Gilya wamesisitiza serikali iwachukulie hatua wale ambao hadi sasa hawajawapeleka watoto wao shuleni.
Wananchi hao wameongeza kuwa kipindi watoto wao wanasoma shule kwa kulipa ada walikuwa wanapata changamoto ya namna ya kuipata ada lakini kwa sasa serikali imewapa urahisi wa kusoma kwa watoto wao bila ya changamoto zozote za kifedha.