Sibuka FM
Sibuka FM
13 June 2025, 5:06 pm

“Hatuwezi kuwavumilia watu au taasisi ya mikopo inayowakandamiza wakopaji kwa kuwatoza riba kubwa ya marejesho na kwa muda mfupi sana ambapo ni kinyume cha sheria na taratibu za mikopo kulingana na vibali vya benki kuu ya Tanzania BOT hivyo lazima tupitishe fagio kwa wakopeshaji makanjanja waotia umasikini familia za wakopaji”.
Na, Daniel Manyanga
Mkuu wa wilaya ya Maswa mkoani Simiyu Dkt. Vicent Anney ametangaza kuanza kwa oparesheni ya kukamata na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria watu na taasisi za mikopo umiza wanaofanya biashara ya mikopo bila kuwa na kibali kutoka benki kuu ya Tanzania BOT hali ambayo inatajwa kuongeza umasikini kwa wakopaji kutokana na kutozwa riba kubwa zaidi hivyo kushindwa kurejesha mikopo kwa wakati.

Dkt.Vicent Anney ametangaza oparesheni hiyo wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo kwa vikundi vya uzalishaji mali vya wanawake,vijana na watu wenye ulemavu kwa awamu ya pili kiasi cha milioni miamoja na thelathini na tatu laki sita na sabini elfu hafla iliyofanyika mapema leo hii katika ukumbi wa halmashauri hiyo.
Awali akisoma taarifa kwa mkuu wa wilaya ya Maswa afisa maendeleo ya jamii wilayani hapo,Lucia Misinzo amesema kuwa halmashauri imeweza kutoa zaidi ya million miamoja thelathini na tatu katika makundi lengwa ya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu hivyo kuongeza kipato kutokana na shughuli wanazozifanya.
Kwa upande wake,Lushinge Salinja, Elizabeth Paul na Salome William ni wanufaika wa mikopo hiyo ya asilimia kumi ya mapato ya ndani ya halmashauri wamemshukuru Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuwaondoa kwenye mikopo umiza au kausha damu.

