Sibuka FM

Bei ya pamba bado ni kitendawili kwa wakulima

3 May 2025, 8:14 pm

Kwenye picha aliyesimama ni mkuu wa mkoa wa Simiyu,Kenani Kihongosi akizungumza jambo na hadhara wakati wa ufunguzi wa manunuzi ya pamba katika msimu wa mwaka 2025/26 Picha kutoka maktaba ya Sibuka fm

‘‘Nani atamfunga Paka kengele? Je nani ambaye ataziona nguvu za wakulima wa zao la pamba wanapohangaika wakati wa kilimo hivi hatuwezi kuwa na soko huria ili kuipa thamani pamba yetu maana naona kabisa vita vya Panzi furaha ya Kunguru anayeumia hapa ni mkulima na siyo mnunuzi kama swala ni soko la dunia basi tuwaruhusu wawekezaji wa viwanda waje nchini ili pamba yetu ilete thamani kwa mkulima ni fikra zangu tu’’.

Na,Daniel Manyanga

Mkuu wa mkoa wa Simiyu Kenani Kihongosi amewataka mameneja na wamiliki wa makampuni yanayonunua pamba mkoani humo kuhakikisha wanazingatia ongezeko la bei ya zao hilo, na kuwalipa wakulima kulingana na bei inavyoongezeka kwa siku husika

Kihongosi ametoa maelekezo hayo wakati akizungumza katika uzinduzi wa msimu wa ununuzi wa pamba wa mwaka 2025/2026 uliofanyika katika mtaa wa Mwakibuga kata ya Nyakabindi wilayani Bariadi  na kuagiza wakulima kulipwa kwa kuzingatia ongezeko la bei.

Sauti ya mkuu wa mkoa wa Simiyu,Kenani Kihongosi akiwataka mameneja wa makampuni ya ununuzi wa pamba kuhakikisha wanatenda haki kwa wakulima
Mkurugenzi mkuu wa bodi ya pamba nchini , Marco Mtunga akiongea na wananchi waliohudhuria hafra ya uzinduzi wa msimu wa manunuzi kwa mwaka Picha kutoka maktaba ya Sibuka fm

Awali akizungumza katika uzinduzi huo mkurugenzi mkuu wa bodi ya pamba nchini, Marco Mtunga amewaasa wakulima wa zao la pamba kuhakikisha wanazingatia kanuni bora za kilimo wanazoelekezwa na wataalam wa kilimo ili kuweza kupata mavuno mengi lengo likiwa ni kuweza kumuona mkulima anapata tija katika zao hilo.

Mkurugenzi wa bodi ya pamba nchini , Marco Mtunga akiwataka wakulima kulima kwa tija ili waweze kujichamua kiuchumi

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Bariadi ,Simon Simalenga amewataka wakulima kuzingatia ubora wa pamba yao hususan kipindi cha mavuno, huku wakulima wakiomba kuongezwa kwa bei ya zao hilo walau ifike shilingi elfu mbili  msimu huu wakieleza kuwa bei iliyotangazwa ni ndogo ikilinganisha na gharama wananzozitumia katika uzalishaji.

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Baraidi,Simon Simalenga akitia neno wakati wa uzinduzi wa msimu wa manunuzi huku wakulima wakiomba bei kuongezwa

Bei ya pamba iliyotangazwa katika uzinduzi huo wa msimu wa ununuzi wa pamba wa mwaka 2025/2026  ni shilingi 1,150 kwa kilo kwa pamba daraja la kwanza na shilingi 575 kwa kilo kwa pamba daraja la pili, bei ambayo imelalamikiwa na wakulima wa zao hilo mkoani Simiyu wakieleza kuwa haitoshi ikilinganishwa na gharama walizozitumia katika uzalishaji na hivyo kuomba bei iongezwe.

Muonekano wa picha za baadhi ya wakulima wakiwa na pamba tayari kwa ufunguzi wa manunuzi ya pamba katika msimu wa mwaka 2025/26 katika viwanja vya kijiji cha Mwakibuga wilayani Bariadi Picha kutoka maktaba ya Sibuka fm