

28 March 2025, 10:11 am
“Hatuwezi kukaa kimya kwa wale ambao walichukua fedha za halmashauri na kwenda kujikwamua kiuchumi lakini linapokuja swala la kurejesha wanaingia mitini haiwezekani halmashauri ibane matumizi kwa ajili ya mikopo halafu watu wasirudishe ifike sehemu wajuwe hizi ni fedha za walipa kodi hivyo watazirudisha “.
Na, Daniel Manyanga
Mkuu wa wilaya ya Maswa mkoani Simiyu,Dkt.Vicent Anney amemtaka mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo kuwasaka na kuwakamata kisha kuwafikisha mahakama vikundi ambavyo havijarejesha mkopo wa asilimia 10 unaotolewa na halmashauri katika makundi ya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu ili kuwainua kiuchumi kupitia mapato ya ndani.
Mkuu huyo wa wilaya Dkt.Vicent Anney ametoa agizo hilo kwa mkurugenzi mtendaji wakati wa hafla ya utoaji wa fedha kwa makundi ya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu ambao ni wajasiliamali kwa awamu ya kwanza kwa mwaka 2025 hafra iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya mkuu huyo wa wilaya ambapo zaidi ya milioni 173 zimekabidhiwa kwa wazalishaji mali hao.
Dkt.Vicent Anney amesema kuwa kunavikundi walikopeshwa hapo nyuma fedha hizo lakini mpaka sasa havijarejesha na hakuna hatua zozote ambazo zimechukuliwa katika kuhakikisha fedha hizo zinarudishwa ili wananchi wengine waendelee kunufaika na mikopo hiyo katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja ndani ya halmashauri.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Maswa, Robert Urassa amesema kuwa hategemei kuona kuna kikundi kinashindwa kurejesha mikopo hiyo ambayo haina riba kwa wale waliofanikiwa kupata mkopo huo kwa awamu ya Kwanza huku akiwataka kuwa mabalozi kwa watu wengine ili nao waweze kunufaika na mkopo wa awamu ya pili kupitia utaratibu wa wezesha kwa kutumia mfumo rasmi wa serikali.